Yohana Paul – Mwanza
TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) Mkoa wa Mwanza, inakusudia kumfikisha mahakamani Ofisa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Boniface Mwasamboma (37) kwa kosa la kuomba na kupokea rushwa kutoka kwa mfanyabiashara anayedaiwa kutokuwa na mashine ya elektroniki ya kutolea stakabadhi (EFD).
Akizungumuza na waandishi wa habari jijini hapa jana, Mwanasheria Mkuu wa TRA Mkoa wa Mwanza, Maxmillian Kyaboya alisema uchunguzi wa Takukuru ulibaini Mwasamboma aliomba rushwa ya Sh milioni moja na kufanikiwa kupokea Sh 400,000 kinyume na kifungu cha 15 (1) a cha sheria ya kuzuia na kupambana na rushwa namba 11 ya mwaka 2007.
Alisema uchunguzi uliofanyika, unaonyesha wakati mfanyabiashara huyo anakamatwa alimuonyeshsa stakabadhi ya kuwa tayari amelipia mashine ya EFD, lakini bado hajapatiwa ambapo pamoja na kufanya hivyo afisa huyo wa mamlaka hiyo alichukua TIN ya mfanyabiashata na kuondoka nayo huku akiomba kiasi hicho cha fedha ili asimfikishe kwenye vyombo vya sheria.
Alisema baada ya kujiridhisha, Takukuru iliandaa mtego na kumukamata Mwasambamo Februari 7, mwaka huu akipokea rushwa ya Sh 400,00.
Alisema uchunguzi wa tuhuma hiyo, umekamalika na anatarajiwa kufikishwa mahakamani janakatika Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Mwanza kujibu mashtaka yanayomukabili.
Katika hatua nyingine, taasisi hiyo inatarajia kuwafikisha mahakamani waliokuwa wafanyakazi wa Mamlaka ya Majisafi na Majitaka Mwanza (Mwauwasa) kwa kosa la matumizi ya nyaraka kwa lengo la kumdanganya mwajiri na kujipatia fedha isivyo halali zaidi ya Sh milioni 26.
Mwanasheria taasisi hiyo, Kyaboya aliwataja watuhumiwa hao, kuwa ni Thobias Abwaro aliyekuwa meneja wa fedha, Daniel Mwita Chegere aliyekuwa meneja ufundi na Michael Kikungo aliyekuwa mhasibu msaidizi.
Alisema watuhumiwa walijipatia fedha hizo baada ya kuandaa hundi tatu tofauti za thamani ya Sh milioni 26.3 kwa maelezo kwamba fedha hizo wamelipia huduma ya umeme kwa Shirika la Umeme Tanzania kwa njia ya malipo taslimu (cash) huku wakijua ni uongo.