Gurian Adolf- Nkasi
WAKAZI wa Kijiji cha Kate wilayani Nkasi mkoani Rukwa, wamekumbwa na taharuki kubwa, baada ya mnyama aina ya nyati kuvamia kijiji hicho na kusababisha wananchi kushindwa kuendelea kwenye shughuli zao.
Akizungumzia tukio hilo jana, Ofisa Mtendaji wa Kata hiyo,Philbert Kwimba alisema nyati huyo alianza kuonekana tangu juzi kijijini hapo, hali iliyosababisha wananchi kushindwa kutoka nje ya makazi yao kuhofia usalama wao.
Ofisa Tarafa wa ya Kate, Bazilio Mazungwa alisema nyati alikutwa nyumbani kwa mfugaji mmoja kijijini hapo juzi saa moja asubuhi, hali iyosababisha wananchi kushindwa kutoka nje ya makazi yao kwa kuogopa kukutana naye.
Alisema kutokana na hali hiyo, walitoa taarifa mamlaka husika ya Serikali kwa lengo la kuomba msaada ili wananchi wa waweze kuendelea na shughuli zao za kawaida.
Alisema hadi sasa hakuna taarifa zozote mbaya zilizoripotiwa tangu nyati huyo kuvamia katika kijiji hicho na wananchi wameendelea kuchukua tahadhari.
Kaimu Ofisa Maliasili na Utalii wa Wilaya ya Nkasi,Frank Wakungwa alisema idara yake kwa kushirikiana na askari wa wanyamapori TAWA wamekwenda eneo la tukio kukabiliana na nyati huyo ili kuondoa hofu inayowakabili wakazi hao.
Alisema kuna namna mbili ya kufanya, kwanza ni kumrejesha nyati huyo ndani ya hifadhi ya Lwafwi alikotoka au kumuua kama ataonekana ni hatarishi kwa usalama wa wananchi.