Na MWANDISHI WETU-DAR ES SALAAM
BENKI ya NMB imezindua akaunti maalumu kwa ajili ya biashara ndogo inayojulikana kama ‘NMB Fanikiwa Akaunti.’
Akaunti hiyo ya aina yake kwa ajili ya biashara ndogo, inatarajia kuwasaidia wafanyabiashara wadogo kama mama ntilie na wamachinga na kuwaingiza kwenye uchumi rasmi.
Kwa mujibu wa benki hiyo, Akaunti ya NMB Fanikiwa ni rahisi kufungua na kuendesha kwa biashara ndogo zenye leseni au vibali na itawezesha wamiliki wake kuingia kwenye uchumi rasmi.
Mkurugenzi Mtendji wa benki hiyo, Ineke Bussemaker, alisema: “NMB Fanikiwa Akaunti ni akaunti maalumu kwa wafanyabiashara wadogo na wa kati.
“Akaunti hii ni mahususi kwa biashara ndogo na zenye thamani kati ya shilingi 500,000 na shilingi milioni 150 kwa mwaka. Hii inaonyesha nia ya dhati ya NMB kutoa huduma zinazoendana na mahitaji ya wateja mbalimbali,” alisema Ineke.
Mkurugenzi huyo alisema NMB ni benki inayohudumia wateja wa aina mbalimbali na imeanzisha akaunti hiyo kwa ajili ya kuwafikishia huduma ya kifedha wale ambao hawajafikiwa.
Alisema kupitia akaunti hiyo wafanyabiashara wadogo na wa kati ambao hawakuwahi kuwa na akaunti ya benki wataweza kujenga uhusiano wa kibiashara na Benki ya NMB na hivyo kuwarahisishia kupata mikopo baada ya kutumia akaunti zao kwa miezi sita
Benki ya NMB imekuwa ikiwahudumia wateja wenye kufanya biashara ndogo na za kati tangu mwaka 2000, ikiwa na lengo la kukuza biashara zao.