NAHODHA wa timu ya Taifa ya Argentina, Lionel Messi, amesema huu ni wakati sahihi wa timu hiyo kutwaa ubingwa wa Copa America.
Nyota huyo wa klabu ya Barcelona, amesema timu hiyo imekaa miaka 23 bila ya kutwaa taji kubwa kama hilo, hivyo ni wakati wa kushirikiana na wachezaji wenzake kwa ajili ya kuchukua ubingwa huo msimu huu.
Msimu uliopita timu hiyo ilifanikiwa kufika fainali ya michuano hiyo dhidi ya Chile, lakini ilijikuta ikitolewa.
“Lazima tupambane msimu huu kuhakikisha tunachukua ubingwa wa Copa America, kwa kuwa tumekaa muda mrefu bila kuchukua hivyo itakuwa muhimu kwetu.
“Ninaamini tunaweza kufanya hivyo mwaka huu kutokana na tulivyo na kikosi bora ambapo tulionesha uwezo katika michuano ya Kombe la Dunia 2014 na kufika fainali ya Copa America nchini Chile. Kwa hali hiyo inaonesha wazi tunastahili mwaka huu kuchukua ubingwa,” alisema Messi.