25.2 C
Dar es Salaam
Tuesday, April 23, 2024

Contact us: [email protected]

Ndayiragije: Safari ya Cameroon bado ipo

THERESIA GASPER-DAR ES SALAAM

KOCHA Mkuu wa timu ya Taifa ya Tanzania ya wanaume ‘ Taifa Stars’ , Etienne Ndayiragije, amesema timu hiyo bado ina nafasi ya kufuzu  Fainali za Mataifa ya Afrika (AFCON 2021)ambazo zimepangwa kuchezwa mwakani nchini Cameroon.

Stars juzi ilishindwa kutamba ugenini, baada ya kuchapwa mabao 2-1 na Libya, katika mchezo wake wa pili wa Kundi J uliochezwa, Uwanja wa Olympique Mustapha Ben Jannet,  Monastir nchini Tunisia.

Libya iliomba kutumia ardhi ya Tunisia kwa ajili ya mchezo wake wa nyumbani dhidi ya Stars, kutokana na kutoimarika kwa hali ya usalama katika nchi hiyo ambayo imeshuhudiwa machafuko tangu utawala wa aliyekuwa Rais wan chi hiyo Marehemu Muamar Gaddafi alipong’olewa madarakani kabla ya kuuwawa.

Matokeo hayo yameifanya Stars kukamata nafasi ya tatu katika msimamo wa kundi J ikiwa na na pointi tatu, wakati Tunisia inakamata usukani ikiwa na pointi sita, Libya ikishika nafasi ya pili ikiwa na pointi tatu sawa na Stars, lakini ikiwa na wastani mzuri wa mabao ya kufunga na kufungwa, wakati Guinea ya Ikweta inaburuza mkia ikiwa haina pointi yoyote.

Akizungumza baada ya mchezo huo, Ndayirage alisema wanayo nafasi ya kumaliza nafasi ya pili kama ya kwanza itashindikana, kwani kwa sasa watapata muda mrefu wa kujiandaa na michezo inayofuata.

“Tumeweza kujifunza mengi kupitia mechi hizi mbili tulizocheza, nimebaini makosa tutaenda kuyafanyia kazi,  niseme kwamba nafasi ya kumaliza nafasi ya pili ipo kama tusipopata ya kwanza,” alisema.

Akizungumzia mazingira ya mchezo wao na Libya kwa ujumla, Ndayiragije alisema; Penalti walipewa wapinzani wetu ilitutoa mchezoni na kusababisha kufungwa bao la pili haraka.

“Tulipata nafasi nyingi kipindi cha kwanza lakini hatukuweza kuzitumia hadi pale tulipopata penalti.

“Kipindi hiki tutapata muda mrefu zaidi wa kujiandaa kabla ya kucheza mchezo mwingine, hili ni jambo zuri kwetu.”

Kikosi cha Stars kilitarajiwa kuwasili nchini usiku wa kuamkia leo kikitokea Tunisia.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles