Mbunge wa Arumeru Mashariki, Joshua Nassari (Chadema), amewasili katika Ofisi ya Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), kwa ajili ya kuwasilisha ushahidi wa awamu ya pili ya tuhuma zinazowahusu madiwani wanane waliohamia Chama cha Mapinduzi (CCM), mkoani Arusha.
Mbali na ushahidi huo lakini pia amefungua jalada la kesi zinazowahusu madiwani hao kama alivyoagizwa na Mkurugenzi wa Takukuru, Valentino Mlowola juzi.
Akiwa ofisini hapo, Nassari alionekana ameshika ‘flash’ na ‘hard disk’ aliyodai ina ushahidi wa tuhuma za madiwani hao.
Nassari na wabunge wengine wa chama hicho, Godbless Lema (Arusha Mjini) na Mchungaji Peter Msigwa (Iringa Mjini) walikwenda ofisini hapo wakidai madiwani wa chama hicho mkoani Arusha na Iringa walishawishiwa kwa rushwa na kuhamia CCM.