24.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Nani kutinga fainali Ligi ya Mabingwa Ulaya wiki hii?

pep-guardiolaNA BADI MCHOMOLO

KIPUTE cha michuano ya Ligi ya Mabingwa barani Ulaya inatarajia kuendelea wiki hii katika hatua ya nusu fainali ya mwisho ambapo lazima apatikane mbabe wa kutinga hatua ya fainali.

Bado kauli ya mtoto hatumwi dukani inaendelea, kwa kuwa wababe wa soka watashuka dimbani na kuonesha soka la ufundi na ubora wa hali ya juu.

Wiki iliopita tuliona wababe hao wanne ambao ni Manchester City, Bayern Munich, Real Madrid na Atletico Madrid walioneshana ufundi ambapo wiki hii wanamaliza ubishi wao na kutarajia wawili kati yao kuyaaga mashindano huku wawili wakitinga fainali ambayo inatarajia kupigwa katika dimba la Giuseppe Meazza kwa jina lingine Uwanja huo unajulikana kwa jina la San Siro uliopo jijini Milan nchini Italia.

Hii itakuwa mara ya nne kwa Uwanja huo kupigwa fainali za michuano ya European Cup, ikiwa mara ya kwanza mwaka 1965, ikifuatiwa na 1970, 2001 na mwaka huu, lakini uwanja huo ulifunguliwa rasmi mwaka 1926, huku ufunguzi ukifanywa na wapinzani wa jiji la Italia, AC Milan na Inter Milan katika uwanja huo ambao unachukua jumla ya watazamaji 81,277.

Mtanzania Kispoti leo hii imekufanyia uchambuzi wa michezo iliopita ya timu hizo na ile ambayo itapigwa wiki hii katika viwanja viwili.

Bayern Munich vs Atletico Madrid

Katika dimba la Allianz Arena ambalo linachukuwa jumla ya watazamaji 75,000, wenyeji Bayern  Munich watawakaribisha wapinzani wao Atletico Madrid katika uwanja huo ambao ulifunguliwa Februari 27, mwaka 1900.

Katika mchezo wa wiki iliopita Bayern walikuwa ugenini lakini walishindwa kutamba chini ya kocha wao wa mipango Pep Guardiola na kukubali kichapo cha bao 1-0 ambacho kiliwapa jeuri wapinzani wao huku wakiamini wanaweza kufanya vizuri wiki hii.

Bao la Atletico linawapa nguvu ya kujiamini kwamba wana nafasi ya kutinga fainali huku mchezo huo wa marudiano ambao utapigwa kesho wakihitaji ushindi au sare ya aina yoyote.

Inaweza kuwa ngumu kwa Atletico kuweza kutamba tena katika jiji la Munich, kwa kuwa Pep Guardiola lengo lake kuondoka Bayern huku akiwa ameacha rekodi mzuri kwa kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu na ikiwezekana kutwaa Ligi ya Mabingwa ambapo fainali yake itapigwa Mei 28 mwaka huu.

Huu ni mchezo ambao utakuwa mgumu zaidi kutokana kila kocha anataka kuweka rekodi, hivyo tunatarajia kuona ufundi wa hali ya juu kwa wachezaji pamoja na makocha wao, wapo ambao wanaamini kwamba Bayern atasonga hatua ya fainali, lakini yote kwa yote ni kesho.

Manchester City vs Real Madrid

Wiki iliopita mchezo wa nusu fainali ya kwanza ulikuwa kati ya Manchester City ambao walikuwa nyumbani kwenye Uwanja wa Etihad na kuwakaribisha Real Madrid kutoka nchini Hispania ambapo mchezo huo ulimalizika kwa sare ya bila kufungana.

Hakika mchezo huu ulionekana kuwa mgumu pale jijini Manchester ambapo ulimalizika bila ya kufungana, wengi waliipa nafasi Real Madrid kushinda mchezo huo, lakini mambo yalikuwa magumu. Ugumu huo ulidaiwa kwamba kumkosa mshambuliaji wao Cristiano Ronaldo ambaye alikuwa majeruhi kuliwapa wakati mgumu.

Japokuwa kulikuwa na Gareth Bale pamoja na Karim Benzema ambaye alikuja kutoka baadae, nao walishindwa kuisaidia timu katika mchezo huo, lakini bado Madrid wanapewa nafasi kubwa ya kufanya vizuri katika mchezo huo wa kesho kutwa ambao utapigwa kwenye dimba la Santiago Bernabeu ambapo Ronaldo atakuwa fiti kuwavaa wageni hao.

Hata hivyo katika mchezo wa awali Manchester City walimkosa kiungo wake hatari Yaya Toure ambaye alikuwa majeruhi lakini safu hiyo ya kiungo ilinogeshwa na David Silva na Kevin De Bruyne, ila katika mchezo huo wa kesho kutwa Silva ataukosa kwa kuwa ni majeruhi lakini Yaya atakuwa ndani na De Bruyne.

Mchezo huu utakuwa mgumu sana ila Madrid wanapewa nafasi kubwa ya kusonga hatua ya fainali japokuwa soka ni mchezo wa makosa, lakini kuna watu wanatabiri kwamba fainali itakuwa ni timu kutoka nchini Hispania, ila ngoja tuone nini kitatokea na nani atatinga fainali.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles