27.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Namna ya kuepuka maumivu kwenye uhusiano

HATA kama utabisha, lakini ukweli utabaki moyoni mwako kwamba mapenzi ni kiungo muhimu katika maisha ya binadamu. Ni lazima uwe na mwenzi.

Huwezi kukwepa, maana hii ni ahadi iliyowekwa na aliyetuumba. Utaweza kuikimbia? Rafiki zangu, wakati tunajadili kuhusu kupenda, kupendwa na kupendana, ndani yake lazima tuzungumzie kuhusu maumivu.

Naam! Machozi na kila aina ya kero. Wakati ukianza uhusiano, kichwani mwako kukiwa na jambo hilo, huwezi kuteseka.

Kikubwa ambacho utaanza nacho ni kutafuta mbinu za kukabiliana na hayo mateso. Kwanini mapenzi yakutese? Kwa nini uyape nafasi hiyo? Mapenzi hayazungumzi, hayana ufahamu hivyo hatupaswi kuyaruhusu yatutese.

Sisi tunapaswa kuyatawala kwa namna yoyote ile, kwa vile tunajitambua. Mapenzi yapo chini ya himaya yetu. Pamoja na yote hayo, bado mapenzi yameendelea kuwa msumari wa moto kwa baadhi ya rafiki zetu.

Kila siku watu wanatafuta namna ya kufurahia mapenzi, lakini majibu yameendelea kuwa sifuri. Katika mada hii tutajifunza mbinu za kuishi kwa amani katika uhusiano wa mapenzi. Si ngumu ni nyepesi sana.

Hebu anza kupitia vipengele vifuatavyo, naamini utajifunza kitu kipya.

UAMINIFU

Hapa nazungumzia uaminifu wako wewe kama wewe. Je, ni mwaminifu au unaishi kama ndege? Unajua mtu ambaye siyo mwaminifu huwa hapendi hata kuonekana hovyo, akipita hapa sasa hivi hutamwona hadi baada ya wiki mbili. Yaani anakwepa watu!

Ukianza kukosa uaminifu wa kawaida hata amani ya moyo wako inakuwa vigumu kuwa nayo. Fikiria kama huna amani na huaminiwi, utaweza kuwa na uaminifu katika mapenzi kweli?

Uaminifu wako kwa mpenzi wako, kuwa wazi kwake kwa kila kitu kunakuweka katika wakati mzuri wa kuyafurahia mapenzi.

Mathalani mpenzi wako akishika tu simu yako roho inakuwa juu, unadhani kutakuwa na furaha katika penzi la aina hiyo kweli? Ni vigumu sana…

Uaminifu ni mwanzo mzuri wa kufurahia mapenzi badala ya kukukera, maana kama wewe si mwaminifu, ukisikia mpenzi wako anakutembelea bila taarifa tayari umeshakuwa mkali na hii ni kwa sababu ya tabia zako za hovyo.

Unadhani muda wowote unaweza kufumaniwa. Kwa staili hiyo mapenzi kwako yataendelea kuwa machungu siku zote za maisha yako. Mateso yatakuwa sehemu ya maisha yako ya kimapenzi.

AMANI YA MAPENZI

Sijui kama umeshawahi kusikia juu ya amani ya mapenzi, lakini kama hujawahi kusikia acha sasa nikuambie kuhusu amani ya mapenzi.

Unaweza kuwa na amani na kila mtu, ukawa na amani mahali pa kazi, lakini ukakosa amani ya mapenzi.

Hili ni tatizo kubwa sana katika maisha ya binadamu maana maisha ya binadamu yametawaliwa kwa kiasi kikubwa na mapenzi, uko hapo?

Usigombane na mpenzi wako kila wakati, usitafute ugomvi usio na maana, wakati wote ishi vizuri na mpenzi wako.

Kama amekukosea mwambie kuliko kumnunia, maana kufanya hivyo hakutakusaidia lolote zaidi ya kuishi bila kuwa na amani ya mapenzi.

Itakuwa ni afadhali zaidi kwenu, maana mtakuwa mmeyazungumza na kuyamaliza hapohapo, halafu maisha yanaendelea kama kawaida. Acha kukaa na vitu moyoni, ni sumu.

KUCHUKULIANA UDHAIFU

Unapokuwa na mwenzi wako ni vyema ukamjua alivyo, vitu anavyopenda na asivyopenda, kwa kujua hivyo ni rahisi sana kumfahamu mpenzi wako yukoje na kitu gani ukikifanya utamuudhi.

Kwa maana hiyo baada ya kumchunguza inawezekana kabisa ukagundua udhaifu wake katika maeneo fulani. Hata kama ana udhaifu katika mwili au siyo mzoefu sana faragha, ana aibu nyingi, hajiamini, siyo mjuaji na mengineyo, usimseme vibaya.

Mfundishe polepole vile ujuavyo wewe ambavyo unajua haviwezi, kwa kufanya hivyo utampa amani ya moyo na utaendelea kuwa na mwezi wako kwa furaha huku akiendelea kuwa mjuzi zaidi katika mambo kadha wa kadha.

Zungumza naye kwa upole, pale alipokukosea mweleweshe kwa mapenzi, acha ukali usiyo na maana, mapenzi ni kubembelezana.

Chukulianeni matatizo yenu na kila mmoja awe mwalimu wa mwenzake. Mateso kwenu yatabaki kuwa historia.

Je, ungependa kujiunga kwenye kundi letu la marafiki la WhatsApp kwa ajili ya kupata zaidi masomo haya? Tafadhali wasiliana na mwandishi inbox ya WhatsApp kwa namba 0718400146, utaunganishwa.

Jiandae kusoma kitabu cha Joseph Shaluwa, SIRI ZA NDOA YENYE FURAHA kitakachoingia mitaani hivi karibuni.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles