28.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

MWENYEKITI WA ZAMANI SIMBA AMKOMALIA MO

Na SOSTHENES NYONI-DAR ES SALAAM

ALIYEKUWA Mwenyekiti wa Baraza la Wadhamini wa  Simba, Hamis Kilomoni, amesisitiza kuwa hakubaliani na mabadiliko ya mfumo wa  uendeshaji wa klabu hiyo.

Klabu ya Simba juzi ilifanya mabadiliko rasmi ya uendeshaji wake ikitoka katika mfumo wa uanachama hadi kuwa wa hisa.

Mabadiliko hayo yalikuwa baada ya wanachama wa Simba  1216 kati 1217 kupiga kura ya kuunga mkono klabu hiyo kuhama kutoka mfumo wa uanachama hadi kuwa wa hisa.

Mfumo huo mpya ambao umefanikisha kuundwa kwa Kampuni ya Simba Sports Club Limited, unatoa fursa kwa wawekezaji kumiliki asilimia 50 ya hisa, huku nyingine 50 zikimilikiwa na wanachama na wapenzi wa klabu hiyo.

Uamuzi huo una maana ya kwamba, sasa njia ni nyeupe kwa mfanyabiashara maarufu na mwanachama wa Simba kununua asilimia 50 zenye thamani ya Sh bilioni 20.

Akizungumza na MTANZANIA jana, Kilomoni alisema  aliulaumu uongozi wa Simba kwa madai kwamba umewadanganya wanachama wa klabu hiyo.

“Msimamo wangu ni ule ule wa kutokubaliana na mabadiliko ya mfumo wa uendeshaji ndani ya Simba, hebu fikiria wanasema watatangaza tenda wakati wanajua tayari wamempa mtu ale sasa huku si kuwadanganya wanachama wa Simba?

“Kwanini suala hili wanalifanya haraka haraka kiasi hicho, kuna nini hapo, wamekutana watu elfu moja wanafanya uamuzi, Simba ina wapenzi zaidi ya milioni 20 nchi nzima, kwa jambo kama hilo walistahili kupata maoni ya watu wengi,” alisema Kilomoni.

Akizungumzia kutimuliwa kwake uenyekiti wa Baraza la Wadhamini wa Simba, alisema bado hajapata barua rasmi hivyo anaendelea na wadhifa wake  kama kawaida.

“Sijapata barua yoyote na naendelea na majukumu yangu kama kawaida na Septemba 4 tunaenda kwenye kesi,” alisema Kilomoni.

Kilomoni aliondolewa kwenye wadhifa huo na Mkutano Mkuu wa Simba uliofanyika jijini Dar es Salaam wiki moja iliyopita, huku pia akisimamishwa uanachama na kutakiwa kujieleza kabla ya kuchukuliwa hatua zaidi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles