MWANDISHI WETU-ZANZIBAR
MKE wa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mwanamwema Shein amesema suala la matunzo ya wazee na ulezi wa watoto linaendeana na utekelezaji wa Sera na Ilani ya Chama cha Mapinduzi (CCM).
Hayo aliyasema jana mjiniUnguja, wakati hafla ya utoaji wa zawadi ya Sikukuu ya Eid El -Hajj kwa wazee na watoto wanaoishi katika nyumba za Wazee Welezo na Sebleni pamoja na vituo vya kutunzia watoto vya SOS na Mazizini, alizozianda kwa kushirikiana na na Mke wa Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Asha Suleiman Idd.
Akizungumza kwa niaba ya Mama Mwanamwema, Waziri wa Wizara ya Kazi, Uwezeshaji, Wazee, Wanawake wa watoto Moudline Castico alisema katika kufanikisha malengo hayo Serikali inatumia zaidi ya shilingi Milioni 200 kwa mwezi, ikiwa ni malipo ya Pensheni jamii kwa wazee wenye umri wa miaka 70 na kuendelea.
“Serikali inaendelea kuyafanyia matengenezo majengo ya makazi ya wazee wasiojiweza ili kuleta ustawi bora wa maisha yao, pamoja na kuwapatia huduma bure za afya ikiwa ni kuthamini mchango mkubwa walioutowa wakati wa ujana wao.
“Pia Serikali inakusudia kuifanya sheria dhana ya Pensheni jamii, ili kuepuka athari za mabadiliko ya uongozi hapo baadae,” alisema
Alisema viongozi hao wameamua kutoa zawadi hizo ili kuhakikisha wazee na watoto hao wanafurahi na kujumuika pamoja na wananchi wengine.
Waziri Castico, aliwataka wazee hao kupitia sikukuu hiyo kuendelea kuliombea dua Taifa, ili liweze kuepukana na athari zitokazo na majanga mbali mbali.
Aidha, aliwataka wazazi na walezi kuzingatia malezi bora na maadili ya ya watoto wao kwa kujiepusha na vitendo vya kikatili na udhalilishaji.
Alisema tukio la hivi karibuni la utupaji wa mtoto Kisiwani Pemba na hatimae kuokotwa na mbwa, linathibitisha kwa kiasi gani jamii isivyojali na kuthamini malezi na mtunzo ya watoto.
Alieleza kuwa Serikali imefanya juhudi kufanikisha upatikanaji wa Mashine ya uchunguzi wa Vinasaba (DNA) ili kukabiliana na wimbi la matukio mbali mbali ya udhalilishaji.
Awali Mkurugenzi wa kituo cha Kulelea watoto cha SOS, Asha Salim aliwashukuru viongozi hao kwa muendelezo wao wa kila mwaka na kuwatakia kheria na afya njema katika amisha yao.