24.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Muhimbili yaokoa bilioni 31 kwa miaka minne

AVELINE KITOMARY -DAR ES SALAAM

MKURUGENZI Mtendaji wa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH), Profesa Lawrence Museru, amesema kuwa hospitali hiyo imeokoa Sh bilioni 32.149 katika kipindi cha miaka minne kutokana na kuanzishwa huduma mbalimbali ambazo zilikuwa hazipatikani nchini.

Profesa Museru akizungumza na waandishi wa habari jana Dar es Salaam kuhusu mafanikio ya miaka minne ya Rais Magufuli, alisema kuwa kiongozi huyo wa nchi amewekeza fedha nyingi katika hospitali hiyo ili kutatua changamoto zilizokuwepo awali na kuanzisha huduma bobezi kupunguza rufaa za nje ya nchi.

Alisema kuwa katika kipindi cha miaka minne Serikali imeweza kuondoa changamoto za uhaba wa dawa, uhaba wa vitanda, kupunguza kero za wafanyakazi na kuanza kutoa huduma bobezi.

“Serikali ya awamu ya tano chini ya Rais Dk. John Magufuli ilipoingia madarakani iliagiza Hospitali ya Taifa Muhimbili kuondoa kero zilizokuwepo kwa wananchi za vipimo kutokufanya kazi, hususani MRI na CT-Scan kutokana na kuharibika kwa muda mrefu, ukosefu wa dawa, uhaba wa vitanda, kulipa stahiki za wafanyakazi ikiwemo posho na nauli za likizo.

“Kutoa huduma za ubobezi ili kupunguza rufaa nje ya nchi, kuboresha mazingira ya kufanyia kazi na kununua na kukarabati vitendea kazi ambapo mpaka sasa tayari kero hizo zimeshatatuliwa ikiwamo matengenezo ya mashine ya CT-Scan na MRI yalifanyika nayo inaendelea kufanya kazi vizuri toka Desemba, 2015 na pia hali ya upatikanaji dawa imeboreshwa ambapo hadi sasa wagonjwa wanapata dawa kwa zaidi ya asilimia 96,” alisema Profesa Museru.

Alisema agizo la utoshelevu wa vitanda limetekelezwa kutokana na kuhama kwa wagonjwa wa Taasisi ya Mifupa (MOI) kutoka wodi za Muhimbili walizokuwa wakitumia ambazo ni wodi 17 na 18 zilizoko jengo la Sewahaji pamoja na wodi namba 2 iliyoko jengo la Mwaisela ambayo kwa sasa ni ICU yenye vitanda 15.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles