29.2 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 24, 2024

Contact us: [email protected]

Mufti atoa ujumbe mzito

CLARA MATIMO- MWANZA

MUFTI na Sheikh Mkuu wa Tanzania, Abubakar Zubeir, amewataka Waislamu waendelee kulinda amani ya nchi kwa kusameheana, kupendana na kushirikiana.

Agizo hilo alilitoa jijini hapa juzi, wakati akizungumza  na mamia ya waumini wa dini hiyo kutoka ndani na nje ya nchi waliohudhuria mkesha wa sherehe za  Maulid ambazo huwa ni kumbukumbu ya kuzaliwa Mtume Mohamad zilizofanyika kitaifa viwanja vya Furahisha.

Alisema mkusanyiko huo, hautakuwa na maana yoyote kama Waislamu wataacha kufuata mwongozo wa  Mtume Muhamad ambao ni kutenda matendo mema katika jamii na kuacha mabaya yote aliyoyakataza mwenyezi Mungu pamoja na Mtume.

“Waislamu wenzangu, nawasihi  muwe wepesi wa kumfuata Mtume yeye ni kioo,  yoyote atakayemfuata  hataharibikiwa bali ataongokewa maana ametufundisha jinsi ya kuishi katika dunia hii.

“Tujenge nguvu katika Uislamu kwa kumuiga Mtume wetu jinsi alivyoishi hapa duniani, alileta amani mahali penye chuki, alisamehe waliomkosea, aliwapenda binadamu wote bila kujali tofauti za dini na alishirikiana nao masuala mbalimbali kwa manufaa ya binadamu wengine.

“Tunapoadhimisha sherehe hizi, nawaacha na ujumbe usemao Waislamu na tabia za Mtume, kila mmoja wetu autafakari kwa kina ujumbe huu, tumswalie Mtume kwa sababu swala yake inaondoa changamoto zetu,”alisema.

Akitoa salamu za maulid kwa niaba ya Rais Dk. John Magufuli, Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, alilipongeza Baraza Kuu la Waislam wa Tanzania( Bakwata) kwa kuwaalika na kushirikiana na Waislam kutoka nchi mbalimbali.

“Bakwata mnastahili pongezi kwa kutambua ujirani mwema unaofanywa na Serikali, maendeleo ya taifa letu yanachagizwa na nchi mbalimbali zikiwamo ambazo leo viongozi wao wa dini mmewaalika na kushiriki nao katika sherehe hizi za Maulid, Serikali itaendelea kuwathamini na kuwaheshimu wananchi wote wa nchi hizo na Serikali zao,” alisema.

Wiki ya Maulid ilizinduliwa rasmi Novemba 4 na Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, John Mongela na imefikia tamati jana.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles