Na SAFINA SARWATT, MOSHI
JESHI la Polisi mkoani Kilimanjaro linamshikilia mtoto Hamis Kayanda (13), mkazi wa Nduruma jijini Arusha, baada ya kuruka ukuta na kuingia ndani ya Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA).
Taarifa hiyo ilitolewa jana na Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro,Wilbord Mutafungwa alipozungumza na waandishi wa habari.
Alisema mtoto huyo alikamatwa na maofisa usalama wa uwanja huo Agosti 20 mwaka huu, saa 2.00 usiku akiwa uwanjani hapo.
“Yule mtoto alipokamatwa alihojiwa na kuwaambia walinzi hao kwamba alikuwa ameacha mkoba wake nyuma ya uzio.
“Kwa hiyo walipofuatilia mkoba huo walikuta pea moja ya viatu vya raba na hakukuwa na kitu kingine cha hatari kama ilivyodhaniwa.
“Baadaye walinzi hao walikagua maeneo yote ya uwanja huo hadi walipojiridhisha kuwa hakukuwa na kitu kingine cha kutisha.
“Lakini bado tunaendelea kumhoji kwa kushirikiana na wenzetu wa Arusha na ikibidi tutaangalia uwezekano wa kumpima akili kabla hatujachukua hatoa zozote,” alisema Kamanda Mutafungwa.