31.7 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Mpina: Tutapiga marufuku samaki wa nje kuingia nchini

Aziza Masoud, Dar es Salaam

WAZIRI wa Mifugo na Uvuvi, Luhaga Mpina, amesema baada ya mwaka mmoja ofisi yake itahakikisha hakuna samaki wanaoingia kutoka nje ya nchi lengo likiwa ni kuongeza kasi ya uvuaji wa samaki  nchini na kupanua soko la biashara hiyo.

Kauli hiyo aliitoa mjini hapa jana wakati wa mkutano wake na wavuvi kutoka maeneo mbalimbali uliokuwa na lengo la kujadili rasimu na kufanya mabadiliko ya Sheria ya Uvuvi namba 22 ya mwaka 2003 na  kanuni zake za mwaka 2009.

Alisema lengo la kufanya mabadiliko ya sheria hiyo itakayoleta sheria mbili yaani Sheria ya Uvuvi ya mwaka 2009 na Sheria ya Ufugaji wa Viumbe Hai ni kutatua  changamoto zilizopo katika sekta hiyo.

“Tunataka tutoe ulinzi thabiti wa rasilimali ili kuwezesha wafanyabiashara wa ndani kuuza samaki na kuacha kuagiza  nje, tunataka baada ya mwaka mmoja habari ya kuagiza samaki kutoka nje ifutike kabisa,” alisema Mpina.

Alisema katika sekta ya uvuvi mambo mengi yanafanyika ikiwamo watu kwenda kuvua kwa gharama kubwa lakini wakifika sokoni wanakuta wa kutoka nje ya nchi na kusababisha samaki wao kukosa soko.

“Samaki wengine wanaingia bila vibali na hata kukaguliwa kwa sababu wamepita njia ya panya, kwanini wapite njia za panya, kwanini waiingie bila kibali, kwanini wananchi wanauziwa na wenyewe wanakubali kula samaki ambao hata hawajahakikiwa ubora wake, kwanini lazima kuna tatizo ambalo jibu lake ni lazima sheria zetu ziwekwe vizuri kwa sababu sisi si wakuagiza samaki nje ni wa kuuza samaki nje ya nchi,” alisema Mpina.

Alisema serikali inataka kudhibiti utoroshwaji wa mazao ya viumbe vya maji  kwa kuwa nchi haiwezi kuwa na maziwa  halafu kinachopatikana kutokana na rasilimali hiyo kinaenda kuuzwa nje ya nchi na nchi isipate chochote.

Alisema marekebisho ya sheria hiyo ni kuimarisha utunzaji wa viumbe vya majini na uwekezaji wake kwa kuwa umekuwa mdogo jambo linasababisha katika bahari kuu kuwa na wavuvi wengi wa kigeni kuliko wazawa.

Alisema lengo lingine la kurekebisha sheria hiyo ni utekelezaji ilani iliyoahidi  kuwateteta na kuwalinda wanyonge  kwa kuwa wavuvi wamekuwa wakifanya shughuli kubwa lakini wanaishi maisha duni.

“Mabadiliko hayo pia yamefanyika ili kwenda sambamba na mabadiliko ya sayansi na tekonolojia huku akitolea mfano wakati tunatunga sheria hii matumizi ya taa za sola hayakuwepo tulikuwa tunatumia karabai,” alisema Mpina.

Pia alisema matatizo ya uvuvi  yaliyopo katika wizara hiyo yanamsababisha anakosa usingizi.

“Yaani ukikaa kwenye hii wizara unashindwa hata kupata usingizi kwa sababu ukitaka kusinzia unaambiwa wavuvi wako wamevua lakini hakuna soko la  samaki, mara samaki wanaoza kwa sababu hakuna wakuwanunua lakini wakati huo huo unaambiwa samaki wanaingia nchini  kinyemela.

“Napo unaambiwa samaki unaowalinda na kuwatunza na uvuvi haramu nao hao hao unaambiwa wanaibwa na kupelekwa nje ya nchi bila kulipa chochote nchini, huwezi  kupata usingizi labda tuje na hii sheria ambayo yote haya yatayalinda kwa nguvu zote,” alisema Mpina.

Kwa upande wa Msemaji wa Chama cha Wavuvi Wadogo Wadogo, Fakya Mbarouk, alisema sheria nyingi za uvuvi zinawakandamiza wavuvi hivyo marekebisho hayo yatakubaliwa kama vipengele kandamizi vitaondolewa.

Alisema miongoni mwa vipengele kandamizi ni pamoja na mvuvi wadagaa  kutoruhusiwa kuvua samaki na mvuvi wa samaki kutoruhusiwa kuvua dagaa endapo akifanya hivyo anakuwa amefanya kosa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles