GLORY MLAY
TIMU ya Mikovila FC inatarajia kushuka dimbani leo kuumana na Mikocheni City, katika mchezo wa ufunguzi wa Ligi Daraja la tatu Wilaya ya Kinondoni utakaochezwa Uwanja wa Mwananyamala, jijini Dar es Salaam.
Akizungumza na MTANZANIA jana, Ofisa Tawala wa Chama cha Soka Wilaya ya Kinondoni (Kifa), Abas Ngau, alisema ligi hiyo itashirikisha timu 28, ambazo zitachezwa kwenye viwanja mbalimbali.
Alisema wanaamini ligi ya msimu ujao itakuwa na ushindani mkubwa kutokana timu nyingi kujitokeza, hivyo akatoa wito kwa wadau wa soka kujitokeza kushuhudia burudani kabambe.
“Kesho (leo) kutakuwa na mechi moja ya ufunguzi wa ligi ambayo itaendelea keshokutwa kwa mujibu wa ratiba, tunawaomba mashabiki wa soka wajitokeze kuwasapoti vijana wetu hawa ambao watakuwa nyota wa baadae,” alisema.
Alisema timu shiriki zimeganywa katika makundi manne, huku akivitaja viwanja vitakavyotumika kuwa ni Kinesi, Magomeni CCM, Msasani, Mwananyamala na TPBC Mikocheni .