28.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

MOHAMED KAMPIRA: MWAMUZI ALIVUNJWA MGUU, WACHEZAJI WATATU WALILAZWA

NA HENRY PAUL



JINA la winga wakulia Mohamed Kampira sio geni masikio mwa wapenzi wa soka nchini hususan wa mkoa waTanga, kwa sababu ameichezea klabu ya Coastal Union ya mkoa huo kwa mafanikio kwa kipindi cha miaka 17 kuanzia mwaka 1975 hadi 1992.

Kampira pamoja na kuichezea klabu hiyo kwa kipindi kirefu cha maisha yake, pia ameichezea timu ya mkoa huo maarufu kama Tanga Stars kwa kipindi cha miaka 10 na timu ya taifa, Taifa Stars kwa miaka mitatu kuanzia 1976 hadi 1979.

Hivi karibuni SPOTI KIKI lilimtafuta mkongwe huyo ambaye hivi sasa amejikita katika kazi ya ukocha na kufanya mahojiano naye kuhusiana na tukio la kusikitisha analolikumbuka zaidi wakati anacheza soka ya ushindani miaka ya nyuma.

Katika mahojiano hayo Kampira tukio la kusikitisha analolikumbuka lililotokea katika mechi ya Kombe la Taifa (Taifa Cup) nusu fainali ambayo ilikuwa ikikutanisha timu yake ya mkoa wa Tanga, Tanga Stars dhidi ya timu ya mkoa wa Dar es Salaam maarufu Mzizima United.

“Tukio hilo la kusikitisha lilitokea katika mchezo wa pili wa marudiano nusu fainali uliochezwa kwenye Uwanja wa Samora mjini Iringa mwaka 1977 ambapo matokeo ni kwamba timu ya mkoa wa Tanga tulifungwa na Mzizima United mabao 2-1.

“Nakumbuka tulicheza mechi hiyo ya marudiano dakika 120 na hata mchezo wa kwanza uliolala tulicheza dakika 120 bila ya mshindi kupatikana.

“Matukio yenyewe ambayo siwezi kuyasahau yaliyosababisha mshika kibendera kuvunjwa mguu na wachezaji watatu kuumizana na hatimaye kulazwa hospitali yalikuwa hivi.

“Mwanzoni mwa kipindi cha kwanza wakati mchezo ukiendelea, mshambuliaji Seleiman Jongo wa Mzizima United wakati anataka kufunga alipamiana vibaya na kipa wetu wa Tanga Stars Staslaus Tadeo na wote wawili kuumia vibaya na kukimbizwa katika hospital ya mkoa wa Iringa kwa matibabu ambapo wote wawili walilazwa.

“Baada ya tukio hilo mchezo uliendelea ambapo katika dakika ya 80 kipindi cha pili wakati mimi nimeisha wapita mabeki Kajole na Mtagwa na kuchanja mbuga kwenda kufunga, alitokea beki wa Mzizima United Mohamed Rishard ‘Adolph’ ambaye alitaka kunikata ‘panga’, lakini nilimwona na kumkwepa na ‘panga’ lile akaenda kumkata mshika kibendera Gyumi kutoka Singida na kumvunja mguu.

“Nakumbuka mshika kibendera mguu wake ulivunjika kabisa kama vile unakata muwa, huku beki ‘Adolph’ yeye akiumia kifundo cha mguu ‘ankle’ na wote wawili kukimbizwa katika hospitali ya mkoa wa Iringa kwa matibabu ambapo wote walilazwa.

“Lakini baadaye wachezaji wa timu zote mbili habari tulizozipa usiku huo ni kwa Jongo na ‘Adolph’ wao waliruhusiwa kutoka hospitalini na kuendelea kujiuguza nyumbani, lakini kipa wetu Tadeo na mshika kibendera Gyumi wao waliendelea kulazwa kwa siku kadhaa.

“Pia tukio lingine la kufurahisha ambalo ninalikumbukwa katika mechi hiyo ni kwamba baada ya kucheza vizuri siku hiyo nilichaguliwa kwa mara ya kwanza kuchezea timu ya taifa, Taifa Stars na aliyekuwa kocha mkuu wa timu hiyo Bert Trautmann kutoka Ujerumani aliyekuwa akisaidiwa na Joel Bendera ambaye hivi sasa ni mkuu wa mkoa wa Manyara.

Kikosi chetu Tanga Stars siku hiyo kiliwakilishwa na Staslaus Tadeo, Mohamed Makunda, Zaharani Makame, Mwihaji Ali, Salim Amir, mimi (Mohamed Kampira), Titus Bandawe, Mohamed Salim, Peter Tino na David Kisingi.

Kikosi cha Mzizima United kiliwakilishwa na Athumani Mambosasa (marehemu), Juma Shabani, Mohamed Kajole (marehemu), Leodger Tenga, Jella Mtagwa, Mohamed Rishard ‘Adolph’, Juma Matokeo (marehemu), Charles Boniface ‘Master’, Hussein Ngulungu na Seleiman Jongo na Adam Sabu (marehemu).

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles