25 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 24, 2024

Contact us: [email protected]

Mnada mali za Mbowe waacha deni

NORA DAMIAN- DAR ES SALAM

MALI za Kampuni ya Mbowe Limited, inayomilikiwa na Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe, zimeuzwa kwa mnada huku Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) likisema litaendelea kumdai kufidia deni analodaiwa.

Mbowe anadaiwa na NHC Sh bilioni 1.1 ambazo ni deni la pango la miaka 20 katika jengo iliyokuwamo clabu ya Bilcanas lililokuwa katika makutano ya barabara ya Mkwepu na Indira Gandhi ambalo ilivunjwa mwaka juzi.

Mnada huo uliendeshwa jana na Kampuni ya Udalali ya Fosters katika Bandari ya Dar es Salaam ambapo MTANZANIA lilishuhudia mali mbalimbali zikiuzwa huku watu wachache wakijitokeza.

MNADA: Wananchi wakiangalia vifaa vya Club Billicanas  iliyokuwa  inamilikiwa na Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe baada ya kupigwa mnada bandarini, Dar es Salaam jana.PICHAl: IMANI NATHANIEL

Katika mnada huo vitu vilivyouzwa kwa bei ya juu ni taa ambazo ziliuzwa kwa Sh milioni 7 na majukwaa yaliyouzwa kwa Sh milioni 5.

Sehemu kubwa ya mali zilizokuwepo eneo hilo ziliuzwa isipokuwa makochi ambayo mnunuzi alitaka kuyanunua kwa Sh 100,000 na dalali akakataa kwakuwa ni bei ya chini.

Mali nyingine ambazo hazijauzwa hadi gazeti hili linaondoka eneo hilo ni jenereta na mashime ya kupoozea (cooling system).

Mkurugenzi wa Kampuni ya Udalali ya Fosters, Joshua Mwaituka, alisema mali nyingi zimeuzwa kwa bei ya chini kwa sababu zimechakaa kwa kukaa muda mrefu. “Mnada hauna bei siku zote wanunuzi ndio wanashindana, sisi tunaangalia anayefika bei ya juu.

“Vitu vingine kama makochi yote yale, mtu anataka kwa Sh 100,000 nimeshindwa kuuza,” alisema Mwaituka.

Naye Meneja wa Kitengo cha Kukusanya Madeni NHC, Japhet Mwanasenga, alisema wanamdai Mbowe Sh bilioni 1.1 na kiasi kitakachosalia baada ya mnada huo wataendelea kumdai.

Hata hivyo Meneja huyo hakuwa tayari kutaja kiasi kilichopatikana jana kwa madai kuwa bado vitu havijaisha.

“Tukishauza fedha iliyopatikana tunaingiza kwenye akaunti na kiasi kilichobaki tunaendelea kumdai,”alisema Mwanasenga.

Kuhusu mali zitakazoshindikana kuuzwa alisema; “Shirika linao utaratibu wake, ikitokea havijauzwa tutagawa hata kwa taasisi za dini kuliko kuuza kwa bei ya chini. Mmoja wa wanunuzi, Mudathiri

Kamanya, alisema alinunua majukwaa kwa Sh milioni 5 na anatarajia kwenda kuyauza kwa mtu mwingine.

Mnunuzi mwingine Abdallah Omary, alisema alinunua majiko, majokofu, viyoyozi na viti kwa kati ya Sh 600,000 na milioni1.6.

Mwaka juzi NHC lilibomoa jengo iliyokuwa Klabu ya Bilicanas ambapo kabla ya ubomoaji huo, Mbowe alipewa siku 14 kulipa deni hilo hata hivyo alishindwa hatua iliyosababisha mali zake kutolewa nje.

Kutokana na hali hiyo, Mbowe kupitia mawakili wake, John Malya na Peter Kibatala, walifungua shauri la kupinga kuondolewa katika jengo hilo Mahakama Kuu ya Tanzania na kutaka kurudishwa katika jengo hilo. Hata hivyo, maombi hayo yalitupiliwa mbali Oktoba 17, 2016 na Jaji Sivangilwa Mwangesi ambaye alisema NHC ilifuata taratibu zote katika kuiondoa Mbowe Hotels Limited.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles