23 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

MKUU WA WILAYA HAI AWAWEKA NDANI VIONGOZI BODI YA MAJI

Na OMARY MLEKWA-HAI


VIONGOZI watatu wa bodi ya wadhamini ya mradi wa maji wa  Water Service Facility (WSF) wilayani Hai wamewekwa ndani saa 48 na Mkuu wa Wilaya hiyo, Lengai Ole Sabaya ili wasiharibu uchunguzi unaoendelea.

Viongozi hao wanatuhumiwa kutumia madaraka vibaya pamoja na kufanya ubadhirifu  wa fedha  za mradi  huo zaidi ya sh. milioni 98.

Ole Sabaya  alitoa agizo hilo baada ya kutembelea ofisi ya mradi huo, na kubaini  ukiukwaji  wa taratibu za uwanzishwaji wa bodi pamoja na matumizi mabaya ya madaraka ya viongozi na kuisababishia serikali ya kukosa mapato yake.

Viongozi waliowekwa ndani kwa saa 48 ni Mhandisi Rojas Marando ambaye ni Meneja, Mwenyekiti wa Bodi, Julias Moleli na  Makamu Mwenyekiti, Yohana Laizer

Pamoja na kuwaweka ndani, Ole Sabaya alitoa agizo la kutafutwa kwa aliyekuwa Mkurugenzi  wa Halmashauri hiyo mwaka 2009, Nicolaus Mtega kutokana na kutumia madaraka ya ofisi vibaya na kuisababishia hasara serikali.

Alisema Mtega alisaidia kuundwa kwa Bodi hiyo kwa manufaa yake binafsi  na baada ya mradi kuisha walijimilikisha kinyume na taratibu huku mkurugenzi huyo akinunua moja ya magari ya mradi kwa sh milioni saba.

Alisema  bodi hiyo tangu mwaka 2012/13 ilikataa kuwasilisha taarifa za fedha pamoja na kukaguliwa kwa madai kuwa haiingiliwi na serikali.

“Mradi huu  serikali ilitoa fedha pamoja na serikali ya Ujerumani kwa ajili ya kusaidia wananchi wa wilaya ya Hai kupata maji lakini umekuwa ukinufaisha watu wawili au watatu, ” alisema.

Pia alimtaka mkurugenzi wa halmashauri hiyo kuchukua mali zote zilizokuwa zikimilikiwa na  WSF na  kuzisimamia .

Aidha alilitaka jeshi la polisi kumtafuta aliyekuwa mhasibu wa bodi hiyo, Devota Mush ambaye anadaiwa kwa kushirikiana na mhandisi ambae ni meneja wa bodi hiyo kuisababishia hasara serikali ya zaidi ya shilinigi milioni 98.

“Watu hawa walikiuka taratibu zote  za manunuzi na baadae wakadai wameibiwa fedha  hizo ambazo  zilikuwa  kwa ajili  ya kuagiza mita za maji, ” alisema Ole Sabaya.

Ole Sabaya pia aliagiza magari manne yaliyokuwa yakitumiwa na bodi hiyo kurudishwa serikalini pamoja na  majengo matatu yaliyokuwa yakitumika kwa ajili ya ofisi na kumbi.

Pia aliagiza eneo hilo kwa sasa lisitumike kwa shughuli zozote hadi hapo muafaka utakapo patikana.

Kwa upande wake , Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo, Yohana Sintoo alisema mradi huo ulijengwa kupitia serikali ya Ujerumani na Tanzania kwa lengo la kuwapatia wananchi wa Hai maji lakini umekuwa ukitumika tofauti.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles