-DAR ES SALAAM
MWENYEKITI wa Bodi ya Wakurungenzi ya Uwekezaji NICOL, Felix Mosha, amesema mkutano wa dharura wa wanahisa wa NICOL uliopangwa kufanyika Oktoba12 mwaka huu, utafanyika kama ulivyopangwa.
Akizungumza jana jijini Dar es Salaam, Mosha ambaye ni mmoja wa waasisi wa NICOL, alisema amelazimika kuitisha mkutano huo ili kutoa taarifa kwa wanahisa kuhusu Sh bilioni nane zilizochotwa na wanaojiita menejimenti ya muda ya NICOL.
Alisema fedha hizo zilikabidhiwa chini ya uongozi wake, hivyo wanalazimika kutolea taarifa kwa wanahisa ili wajue hatua za kuchukua.
“Lengo la mkutano huo wa dharura ni kutoa taarifa kwa wanahisa kuhusu kutolewa kwa zaidi ya Sh bilioni nane za wanahisa kutoka kwenye akaunti ya NICOL iliyoko NMB. Fedha hizo zilitolewa na wanaojiita menejimenti ya muda ya NICOL wakati hawakuwa wanaendesha kitengo chochote NICOL ambacho kingehitaji matumizi ya uendeshaji,” alisema.
Mwenyekiti huyo wa NICOL alisema kuwa amelazimika kutoa msisitizo wa kuwapo kwa mkutano huo kutokana na kile alichoita kuwa propaganda alizodai zinaendeshwa na baadhi ya watu kubeza na kupinga mkutano huo.
Alisema hadi sasa taratibu za mkutano huo zinaendelea na kwamba utafanyika katika viwanja vya Karimjee jijini Dar es Salaam na kuongeza kuwa mwanahisa atakayeshindwa kuhudhuria atume jina la atakaye mwakilisha pamoja na hati ya hisa za anayewakilishwa.
Akitoa ufafanuzi kuhusu historia ya NICO, Mosha alisema Machi 11 mwaka 2011, Mamlaka ya Mitaji na Dhamana (CMSA) iliioondoa bodi ya NICOL kinyume cha sheria ambayo ilichaguliwa kihalali na kukabidhiwa amana za wanahisa chini ya uongozi wa Mosha na mtendaji Mkuu (CEO), Kathleen Armstrong.
Alisema Machi 6 2012, Mahakama Kuu ilitoa amri iliyoirudisha bodi hiyo na CEO wake katika nafasi zao NICOL na amri hiyo haijawahi kutenguliwa na Mahakama ya juu zaidi hadi sasa.
Mosha alisisitiza kuwa mkutano huo ni wa dharula, hivyo ni muhimu kwa wanahisa kuhudhuria ili kujua hatua za kuchukua kuhakikisha NICOL inasonga mbele.