23 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

MKURUGENZI CIA AZURU KWA SIRI KOREA KASKAZINI

WASHINGTON, MAREKANI


MKURUGENZI wa Shirika la Upelelezi Marekani (CIA), Mike Pompeo, alisafiri hadi mjini Pyongyang kwa mkutano wa kisiri na Kiongozi wa Korea Kaskazini, Kim Jong Un kwa mujibu wa vyombo vya habari vya Marekani.

Mkutano huo, ambao ni sehemu ya maandalizi ya ule wa baina ya Rais wa Marekani, Donald Trump na Kim ulifanyika mwishoni mwa wiki wakati wa Sikukuu ya Pasaka.

Trump mwenyewe alikuwa amekiri bila kufafanua kufanyika kwa mazungumzo ya hadhi ya juu na Pyongyang.

“Tumekuwa na mazungumzo ya moja kwa moja, katika ngazi za juu,” Trump alisema mjini Florida ambako alikuwa anakutana na Waziri Mkuu wa Japan, Shinzo Abe.

Rais huyo aliongezea kuwa aliunga mkono mazungumzo kati ya Korea Kusini na Kaskazini kuzungumzia makubaliano ya amani ya kumaliza vita ya Korea ya 1950-1953.

Korea Kusini imetoa ishara kuwa itaangazia suluhu rasmi ya kumaliza mgogoro huo, huku Rais wa Korea Kusini, Moon Jae in na Kim wakitarajiwa kukutana mwisho wa Aprili.

Habari kuwa mteule huyo wa Rais Trump wa uwaziri wa mambo ya nje alisafiri kwenda Korea Kaskazini kuonana na Kim, ziliripotiwa mara ya kwanza na gazeti la The Washington Post la hapa.

Ni machache yanayojulikana kuhusu mazungumzo hayo mbali ya kuwa ni jukwaa la kuandaa mkutano mwingine wa moja kwa moja baina ya Trump na Kim.

Kwa mujibu wa gazeti hilo, mkutano huo ulifanyika mara tu baada ya Pompeo kuteuliwa kuwa Waziri wa Mambo ya Nje.

Safari ya Pompeo ilikuwa ya kwanza ya ngazi Marekani nchini Korea Kaskazini tangu mwaka 2000 wakati aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, Madeleine Albright alipokutana na Kim Jong-il, baba wa kiongozi wa sasa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles