Nairobi, Kenya
 Mke wa Rais wa Marekani Donald Trump, Melania Trump, amewasili Kenya, jana Alhamisi jioni kwa ziara ya siku moja ikiwa ni nchi ya tatu kuitembelea katika ziara yake ya kwanza barani Afrika.
 Melania, baada ya kuwasili amepokelewa na mke wa Rais wa Kenya, Margaret Kenyatta, katika uwanja wa ndege wa kimataifa wa Jomo Kenyatta (JKIA).
Leo anatarajiwa kutembelea sehemu mbali mbali ikiwa ni pamoja na kituo cha kuhifadhi wanyama pori cha David Sheldrick, Ukumbi wa Taifa wa Sanaa jijini Nairobi kujionea kazi za uigizaji na utamaduni wa Kenya kisha aelekee ikulu kwa mazungumzo.
Kabla ya kuwasili Kenya,  Melania, alianza ziara yake nchini Ghana, mapema wiki hii kabla ya kwenda Malawi.
Ziara ya Melania Trump, nchini Kenya, inafuatia mashauriano waliyofanya na Mke wa Rais wa Kenya, Margaret Kenyatta, katika Ikulu ya Marekani wakati alipoandamana na Rais Uhuru Kenyatta, katika ziara ya mwezi Agosti, mwaka huu huko mjini Washington DC.