25.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Miili ya watu wanne yaokotwa Mongolandege

Christina Gauluhanga -Dar Es Salaam

WAKAZI wa Mongolandege wametakiwa kuchukua tahadhali kwa kuacha kuvuka mto Msimbazi katika kipindi hiki cha mvua kwa sababu ya usalama wa maisha yao.

Akizungumza na MTANZANIA Mwenyekiti wa Serikali ya mtaa huo (CCM), Rajab Tego amesema, kipindi hiki ni kigumu hivyo ni vema wananchi wakatumia njia nyingine mbadala kwenda kwenye shughuli zao za kila siku.

Alisema kutokana na Mto Msimbazi kujaa kwa sababu ya mvua zinazoendelea kunyesha kuna miili ya watu wanne imeokotwa na kupelekwa Hospitali ya Taifa Muhimbili kuhifadhiwa.

“Kwa yeyote atakayekuwa amepotelewa na ndugu yake katika kipindi hiki ni vema akaenda Hospitali ya Taifa Muhimbili ili kuitambua miili hiyo,” alisema Tego.

Tego alisema pia amepokea taarifa za watu wanne kusombwa maji katika Mto Msimbazi akiwamo mama aliyebeba mtoto aliyetumbukia mtoni na kusombwa .

“Ninawaomba ndugu zangu tupeane taarifa za mara kwa mara  kuhusu matukio mbalimbali yanayojitokeza katia kipindi hiki ikiwa ni pamoja na kuepuka kuvuka mto Msimbazi kwa sasa pindi mvua ina[ponyesha kwakuwa maji yanajaa kiasi cha kutishia usalama wa maisha hasa kwa wakazi wanaovuka kwenda kwenye shughuli zao mbalimbali,” alisema Tego.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti baadhi ya wananchi waliiomba Serikali kuchukua jitihada za haraka kujenga daraja la Ulongoni na Mongolandege kwakuwa wamekuwa wakipata adha wakati wa kwenda kwenye shughuli zao pamoja na wanafunzi wanavyokwenda shule.

“Daraja la Mongolandege ni zaidi ya miaka 10 sasa lilisombwa na mvua wananchi tumekuwa tukiteseka ikiwa ni pamoja na kulipa gharama kubwa ya nauli jambo ambalo ni hatari hata kwa usalama wetu,” alisema Jumanne Mussa.

Mussa alisema ukosefu wa daraja hilo umesababisha hata gharama za vyakula kupanda kwa sababu wengi wanatumia mwanya huo kufidia gharama za kusafirisha bidhaa zao.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles