RAMADHAN HASSAN – DODOMA
MFUMUKO wa bei kwa mwaka ulioishia Agosti 2019 umepungua hadi kufikia asilimia 3.6 kutoka asilimia 3.7 Julai 2019.
Hayo yalielezwa juzi jijini hapa na Mkurugenzi wa Sensa za Watu na Takwimu za Jamii, Ruth Davison, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari.
Alisema mfumuko wa bei wa taifa unapima kiwango cha kasi ya mabadiliko ya bei za bidhaa na huduma zote zinazotumiwa na kaya binafsi nchini.
“Hii inamaanisha kuwa kasi ya mabadiliko ya bei za bidhaa na huduma kwa mwaka ulioishia Agoati 2019 umepungua ikilinganishwa na kasi iliyokuwepo Julai 2019,” alisema.
Alizitaja baadhi ya bidhaa zisizo za vyakula zilizopungua bei kwa Agosti 2019 zikilinganishwa na bei za Agosti mwaka jana ni pamoja na mafuta ya taa kwa asilimia 2.6, petroli kwa asilimia 4.3, maji ya gesi kwa asilimia 1.4, gharama za kufanya ukarabati wa nyumba kwa asilimia 1.7 na bidhaa za usafi binafsi kama mafuta ya nywele kwa asilimia 1.3.
Alisema kwa upande wa mfumuko wa bei wa bidhaa za vyakula na vinywaji baridi kwa mwezi Agosti 2019, umeongezeka hadi kufikia asilimia 3.7 kutoka asilimia 2.9 Julai 2019.
Pia alitaja hali ya mfumuko wa bei kwa nchi za Afrika Mashariki ambapo alisema nchini Kenya kwa mwaka ulioishia Agosti 2019 umepungua hadi asilimia 5.00 kutoka asilimia 6.27 kwa mwaka ulioishia Julai 2019.
Kwa upande wa Uganda, mfumuko wa bei kwa mwaka ulioishia Agosti 2019 umepungua hadi asilimia 2.1 kutoka asilimia 2.6 kwa mwaka ulioishia Julai 2019.