MEXICO CITY, MEXICO
MAELFU ya watu wameandamana katika miji mbalimbali nchini Mexico kupinga mpango wa Serikali wa kuhalalisha ndoa za jinsia moja.
Makundi ya kihafidhina yakishirikiana na maskofu kadhaa waliitisha maandamano hayo katika miji ya Mexico City, Veracruz, Puebla na mingineyo.
Kwa mujibu wa waandaji wa maandamano hayo, watu wapatao 300,000 walijitokeza kushiriki.
Mwaka jana, mahakama ya juu ya taifa hilo lenye wingi wa waumini wa Kikiristo wa madhehebu ya Kikatoliki, ilisema kupigwa marufuku kwa ndoa za jinsia moja ni kinyume na masharti ya demokrasia.
Kwa sababu hiyo, Rais wa Mexico, Enrique Pena Nieto ameitaka serikali yake kuifanyia marekebisho katiba ya nchi na kuruhusu ndoa za mashoga nchini kote, kitu ambacho wakosoaji hao wanakipinga vikali.