23.9 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 24, 2024

Contact us: [email protected]

Mbunge Chadema apandishwa kizimbani

Joshua Nassari
Joshua Nassari

NA JANETH MUSHI, ARUSHA

MBUNGE wa Arumeru Mashariki, Joshua Nassari (Chadema) na madiwani wanne wa Halmashauri ya Wilaya ya Meru, wamepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha kwa tuhuma za kuharibu mali kwa makusudi.

Nassari na wenzake hao walifikishwa mahakamani hapo jana na kuunganishwa katika kesi iliyopo.

Juni 8 mwaka huu, madiwani 24 wa Chadema wakiongozwa na Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo, Willy Njau, walifikishwa mahakamani hapo kwa tuhuma hizo.

Mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama hiyo, Agustino Rwizile, Wakili wa Serikali, Gaudensia Joseph, aliiomba mahakama hiyo kufanya marekebisho kwenye hati ya mashitaka kwa kuwaongeza washitakiwa hao watano na kufanya idadi ya washitakiwa katika kesi hiyo kuwa 29.

Aliwataja washitakiwa wengine kuwa ni Paulo Shango, Japhet Jackson, Zephanja Mwanuo na Anderson Sikawa.

Akiwasomea shitaka linalowakabili, Wakili Gaudensia alidai   kuwa Mei 4 mwaka huu, watuhumiwa hao kwa pamoja waliharibu uzio wenye thamani ya Sh milioni saba,   mali ya Itandumi Makere.

Kwa mujibu wa Gaudensia, tukio hilo lilitokea katika eneo la Usa River, Leganga na kwamba lilifanywa kinyume na kifungu cha 326 (1) cha kanuni ya adhabu.

Washtakiwa hao wanaotetewa na Mawakili  Charles Abraham na Gift Joshua, walikana mashitaka na kuachiwa baada ya kujidhamini kwa hati ya Sh milioni moja na kuwa na mdhamini atakayesaini hati yenye thamani ya Sh milioni moja pia.

Watuhumiwa wengine katika kesi hiyo ni  Makamu Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo, Nelson William, Elisa Stephen, Digna John, Dina Erick, Wilson Fanuel, Josephine Anael, Samuel Ismail, Agness Eliya, Isack Afitwe na Neema Isack.

Wengine ni Gadiel Stanley, Jeremia Masawe, Peter Efatha, Benard Wilson, Henry Benjamin, Emanuel Pendaeli, Fadhila Joseph, Penzila Palangyo, Mery Antony, Roman Laurance, Bryson Mosses, Frank Ngoye na Eveline Julius.

Wakili wa Serikali alidai   upelelezi wa kesi hiyo  haujakamilika na shauri hilo liliahirishwa hadi Juni 28 mwaka huu  litakapoendelea.

Halmashauri ya Meru ilikuwa na diwani mmoja wa CCM katika Kata ya Ngarenanyuki, Naftal Mbise aliyefariki hivi karibuni. Kata nyingine 17 zinaongozwa na Chadema.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles