23 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

Mbunge amtisha DC Karagwe

Na Arodia Peter, Dodoma
MBUNGE wa Karagwe (CCM), Gozibert Blandes, amemtishia kumfanyia kitu kibaya Mkuu wa Wilaya ya Karagwe, Dari Rwegasira, kutokana na kuwapendelea wahamiaji haramu kutoka Rwanda.
Mbali na hilo pia mbunge huyo ameitaka Serikali kumhamisha.
Blandesi alitoa vitisho hivyo bungeni jana wakati akichangia bajeti ya ofisi ya Waziri Mkuu kwa mwaka 2015/2016.

Alisema Rwegasira amekuwa mstari wa mbele kunyanyasa wananchi kwa kuwanyang’anya ardhi katika vijiji vilivyo mpakani na nchi ya Rwanda huku akiwapendelea wahamiaji haramu.

“Mwenyekiti, DC huyu ni bomu, ni mzigo, yeye anafanya kazi huku mwili ukiwa Tanzania lakini roho yake ikiwa Rwanda, ninaomba Serikali msiwe mnatuletea watu waliochoka kiasi kile.
“Huyu mama DC amechoka na anakaribia kustaafu, anadhani mbunge anafanya kazi chini yake, hajui kama mimi ninapaswa kumsimamia. Na ninasema kama hamtamwondoa mtaona tutakachokifanya” alisema Blandes.
Hata hivyo kabla ya Bunge kuahirishwa mchana, Mbunge wa Viti Maalumu mkoani Mara, Rose Kirigini, alisimama kuomba mwongozo kuhusu kauli hiyo ya Blandes.
Kirigini ambaye pia ni Mkuu wa Wilaya ya Meatu mkoani Shinyanga alitumia Kanuni namba 68 (7), inayosema mbunge yeyote anaweza kusimama na kuomba mwongozo wa jambo lililojitokeza wakati wa majadiliano.
“Mheshimiwa mwenyekiti, wakati wabunge wakiendelea kujadili hotuba ya waziri mkuu limejitokeza jambo ambalo linasononesha na kusikitisha.
“Kwanza naomba kutangaza maslahi kwamba mimi ni mkuu wa wilaya lakini vilevile ni mbunge.
“Katika bunge lako tleo Mbunge wa Karagwe ametoa lugha ya vitisho na uchochezi mkubwa dhidi ya DC wa Karagwe, nilikuwa naomba mwongozo wako.
“Kwa kuwa DC wa Karagwe tunatambua kwamba ni msimamizi mkuu wa amani na hata yeye yuko hapa ndani na kwa kutambua nafasi yake kwamba ndiye mkuu na mwakilishi wa ulinzi na usalama na ndiye mwakilishi wa rais kule wilayani, naomba mwongozo wako,” alisema Kirigini.
Baadaye Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Uratibu na Bunge, Jenista Mhagama, alisimama na kusema wamesikia malalamiko ya Kirigini na Ofisi ya Waziri Mkuu ndiyo ina ratibu shughuli zote za serikali ndani na nje ya Bunge kwa hiyo waachiwe watalifanyia kazi kwa taratibu zitakazokwenda kupima pande zote mbili na hatua zitachukuliwa.

Baada ya Mwenyekiti wa Bunge, Mussa Azzan Zungu, kuahirisha kikao hicho mchana, Blandes na baadhi ya wabunge wa Kagera walikuwa wakizungumza ingawa haikujulikana mara moja mazungumzo yao yalihusiana na nini.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles