27.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Mawaziri wapanga kumwondoa Waziri Mkuu Uingereza

LONDON, UINGEREZA

VYOMBO vya habari nchini Uingereza vinaripoti kuwa mawaziri wamekataa kuunga mkono uongozi wa Waziri Mkuu Theresa May na wanamtaka aachie madaraka.


Hatua hiyo ya uasi ndani ya baraza lake mwenyewe la mawaziri inakuja siku chache kabla ya kura ya tatu kuhusu makubaliano ya May juu ya Brexit yaliyokataliwa mara mbili.


Magazeti ya The Sunday Times, The Telegraph na The Daily Mail jana yaliripoti juu ya uwezekano wa mapinduzi, yakiwanukuu wabunge wa Chama chake cha Conservative.


Inasemekana kiongozi wa muda atachaguliwa kusimamia wiki za mwisho za mchakato wa Brexit.
Gazeti la udaku la The Daily Mail lilisema Waziri wa Mazingira, Michael Gove huenda akachukua uongozi wa mpito kabla ya kinyang’anyiro kamili wakati wa msimu wa joto.


Mhariri wa Siasa wa Gazeti la The Times Tim Shipman alisema mawaziri wamemgeuka May kwa namna ya kushangaza, na wanamshinikiza aondoke mara moja, ingawa bado hawajachukua uamuzi thabiti kufanya hivyo.


Aliongeza kuwa mume wa May alikuwa moja wa wachache wanaomhimiza aendelee kuwepo kama waziri mkuu.
Mbunge anayeunga mkono Brexit, Anne-Marie Trevelyan alilieleza gazeti la The Telegraph namna May alivyoruhusu kutendewa mjini Brussels ilikuwa dhihaka na hivyo azma ya kurejesha udhibiti.


Mtandao wa Buzzfeed News ulisema Mnadhimu wa Serikali, Paul Maynard alimuambia May kuwa mkakati wake ulikuwa umeshindwa na unakiharibu chama chao.


Mapema siku ya Jumamosi, zaidi ya watu milioni moja waliandamana katika mitaa ya jiji la London kudai kura ya pili ya maoni, na kuhimitisha miaka miwili ya mashaka ya kisiasa.


Mabango yalikuwa na ujumbe kwa serikali kama vile kuondoa kifungu cha 50 na ‘tunaandamana kutaka kura ya watu na pia Tunaupenda Umoja wa Ulaya.’


Maandamano hayo yalihudhuriwa na watu kutoka vyama vyote ambapo Naibu Kiongozi wa Chama cha Labour, Tom Watson alisema anaunga mkono kura ya pili ya maoni kama njia pekee ya kutatua mkwamo wa Brexit.


Pia Waziri Kiongozi wa Scotland, Nicola Sturgeon na Kiongozi wa chama cha Liberal Democrats Vince Cable walishiriki maandamano hayo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles