29.2 C
Dar es Salaam
Wednesday, April 24, 2024

Contact us: [email protected]

MAUZO SOKO LA HISA DAR YAPUNGUA

Na JOHANES RESPICHIUS-DAR ES SALAAM



MAUZO ya hisa katika Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE), yameshuka kutoka Sh bilioni nne wiki iliyopita hadi Sh bilioni 3.7 wiki hii.
Hiyo imeelezwa kuwa imechangiwa na kushuka bei ya hisa za baadhi ya makampuni yaliyoorodheshwa sokoni hapo.
Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Ofisa Mwandamizi wa Masoko wa DSE, Mary Kinabo, alisema pamoja na kushuka huko, idadi ya hisa zilizouzwa na kununuliwa ilipanda kutoka milioni 7.6 hadi milioni nane.
Alisema kampuni zilizoongoza katika mauzo ya hisa zake ni Kampuni ya Bia Tanzania (TBL) kwa asilimia 63, ikifuatiwa na Benki ya CRDB asilimia 34 na DSE asilimia mbili.
“Ukubwa wa mtaji wa kampuni zilizoorodheshwa sokoni umepungua kwa Sh bilioni 433 kutoka Sh trilioni 21 hadi Sh trilioni 20.8.
“Hii ni kutokana na kushuka kwa bei za hisa za Uchumi Supermarket Ltd (USL) asilimia 10, Acacia Mining (ACA) kwa asilimia 10, Kenya Commercial Bank (KCB) asilimia 5 na DCB asilimia 1.
“Ukubwa wa mtaji wa kampuni za ndani umepanda kwa Sh bilioni 88 kutoka Sh trilioni 10.037 hadi kufika Sh trilioni 10.13 ikichangiwa na kupanda kwa bei ya hisa ya TBL kwa asilimia 2,” alisema Mary.
Kuhusu viashiria vya soko, Mary alisema kiashiria cha kampuni zilizoorodheshwa sokoni ,yaani DSEI kilipungua kwa pointi 45 kutoka 2,207 hadi 2,162 ikiwa ni kutokana na kushuka kwa bei za hisa za USL, ACA, KCB na EABL.
“Kiashiria cha kampuni za ndani, yaani TSI, kimepanda kwa pointi 34 kutoka 3,829 hadi 3,862 kutokana na kupanda bei za hisa za Tanzania Breweries Ltd (TBL), hivyo hivyo kwa sekta ya viwanda iliyopanda kwa pointi 78 kutoka 5,293 hadi 5,372.
“Pia kiashiria huduma za benki na fedha kimepanda kwa pointi 0.44 kutoka 2,461 hadi 2,461.44, huku sekta ya huduma za biashara ikibaki kama awali kwenye wastani wa pointi 2,462,” alisema Mary.
Alisema mauzo ya hati fungani yalishuka kutoka Sh bilioni 17 hadi Sh bilioni 1.4 baada ya kuuzwa kwa hati fungani tano za Serikali zenye thamani ya Sh bilioni 1.6 kwa gharama hiyo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles