31.2 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

MAUAJI YA WATAFITI YAONDOKA NA VIGOGO POLISI

KAMANDA wa Polisi Mkoa wa Dodoma, Lazaro Mambosasa
KAMANDA wa Polisi Mkoa wa Dodoma, Lazaro Mambosasa

Na ASHA BANI-DAR ES SALAAM

KAMANDA wa Polisi Mkoa wa Dodoma, Lazaro Mambosasa, amewachukulia hatua maofisa wawili wa ngazi za juu wa jeshi hilo kutokana na kushindwa kushughulikia tukio la mauaji ya watafiti watatu waliouawa Oktoba 2, mwaka jana.

Mauaji ya watafiti hao yaliyofanywa na baadhi ya wakazi wa Kijiji cha Iringa-Mvumi, Chamwino mkoani Dodoma, yamewafikisha maofisa hao mbele ya mahakama ya kijeshi, Mkuu wa Upelelezi wa Wilaya ya Chamwino (OCCID) na Mkuu wa Polisi wa Wilaya (OCD).

Watafiti waliouawa na wananchi kwa kuchomwa moto ni Jafari Mafuru, Theresia Ngume na Nikas Magazine ambao walikuwa wametokea Kituo cha Utafiti wa Udongo na Maendeleo cha Selian, jijini Arusha.

Kamanda Mambosasa alisema hatua walizochukuliwa OCCID na OCD ni kuvuliwa nyadhifa zap, huku wakiwa wanaendelea kujibu mashtaka mbele ya mahakama hiyo.

Alisema OCCID aliyemvua madaraka atapangiwa kazi nyingine na OCD hana mamlaka naye ingawa wote wanashtakiwa kwenye mahakama ya kijeshi kutokana na jinsi walivyoshughulikia tukio hilo.

Kamanda Mambosasa alisema askari polisi hao wawili wa Kituo cha Mvumi, siku ya tukio walifika eneo la tukio kabla watafiti ambao kwa sasa ni marehemu hawajashambuliwa, lakini walishindwa kuokoa maisha yao.

“Licha ya kwamba walishindwa kuokoa maisha yao, lakini walirusha risasi walizokuwa nazo hewani bila mafanikio,’’ alisema Kamanda Mambosasa.

Alisema uchunguzi uliridhisha kuwa kitendo cha askari hao kukimbia na kutelekeza pikipiki yao eneo la tukio, ndicho kilichonusuru maisha yao, na kwamba endapo wangefanya tendo lolote tofauti na hilo nao wangepoteza maisha.

Pamoja na viongozi hao wa polisi, hadi Desemba mwaka jana wanakijiji 39 walikuwa wamefikishwa mahakamani wakituhumiwa kwa mauaji hayo.

Kesi hiyo inaendelea kutajwa mbele ya Hakimu Mkazi wa Mkoa wa Dodoma, Joseph Fovo huku watuhumiwa wakitakiwa kutojibu chochote kutokana na mahakama hiyo kutokuwa na mamlaka ya kisheria kusikiliza shauri hilo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles