24.7 C
Dar es Salaam
Tuesday, March 19, 2024

Contact us: [email protected]

Matic afunguka sababu ya kufungwa na Everton

LONDON, ENGLAND

KIUNGO wa timu ya Manchester United, Nemanja Matic, amesema kikosi chao kilikosa kiongozi ndani ya uwanja wakati kikishushiwa kichapo cha mabao 4-0 kutoka kwa Everton kwenye Uwanja wa Goodison Park.

Lakini Manchester United bado ina matumaini ya  kutinga nafasi ya nne kwenye msimamo wa  Ligi Kuu England, licha ya kipigo hicho cha mabao kutoka kwa  Richarlison, Gylfi Sigurdsson, Lucas Digne  na Theo Walcott.

Manchester United imepoteza michezo sita  kati ya minane kwenye michuano yote  tangu ifanye vizuri katika Ligi ya Mabingwa Ulaya dhidi ya PSG mwezi uliopita.

Matic anakiri kwamba  anastahili lawama  kutokana  na kucheza chini ya kiwango akiwa miongoni mwa wachezaji wachache wenye uzoefu ndani ya kikosi cha timu hiyo.

“Nafikiri  mambo  hayakwenda kama tulivyotarajia leo (juzi).

“Tulijiandaa na mchezo kama ambavyo tunafanya kila siku. Benchi la ufundi lilituonyesha kila eneo ambalo Everton wangekuwa hatari kwetu lakini nafikiri tatizo kubwa hatukuwa na kiongozi ndani ya uwanja leo.

“Mimi ni mchezaji mzoefu kwenye timu, hivyo kama hatukufanya vizuri  eneo la kiungo inakuwa ngumu wachezaji wengine kucheza. Na kama kuna mtu anatakiwa kulaumiwa, basi nitakuwa wa kwanza.

“Nafikiria vitu vingi, lakini ni jambo jema kuwa na utulivu wa akili ya  ushindi ndani ya chumba cha kubadili nguo.

“Ni rahisi kusema kwamba ukishinda unakuwa na utulivu wa akili, lakini wakati ukipoteza watu wanataka kufahamu tatizo na nina uhakika watachambua kila kitu na watapata njia sahihi ya kutatua tatizo,” alisema Matic.

Manchester United inakabiliwa na kibarua kingine kigumu dhidi ya Manchester City ambao wapo kwenye mbio za ubingwa msimu huu.

Matic anaamini kuwa  Manchester United itacheza kwa jihadi kushinda mchezo huo.

“Aina hii ya mchezo nafikiri tutakuwa na hali ya ushindi. Kwenye mchezo huu si tatizo kwa timu yetu kutafuta hali ya ushindi.

“Tatizo wakati unacheza dhidi ya timu ambayo siwezi sema ndogo lakini haipo kwenye nafasi sita za juu ya msimu wa ligi. Pia msimu uliopita tulikuwa kwenye tatizo kama hili dhidi ya timu iliyokuwa katikati ya msimamo wa ligi ambayo ilikuwa ikitafuta kuepuka kushuka daraja,” alisema Matic.

Baada ya kupoteza mchezo huo, Manchester United  imebaki nafasi ya sita kwenye msimamo wa Ligi Kuu England, huku ikiwa imepitwa pointi mbili dhidi ya Arsenal ambayo ipo nafasi ya nne.

Michezo mingine iliyobaki kwa Manchester United ni dhidi ya Chelsea, Huddersfield na Cardiff.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
584,000SubscribersSubscribe

Latest Articles