WASHINGTON, MAREKANI
SERIKALI za Marekani na Urusi zimeendelea kupambana vikali juzi kuhusiana na jinsi ya kuisaidia Venezuela iliyokumbwa na mzozo wa kisiasa, ambapo Urusi iliamua kutoa njia mpya za kutoa misaada kupitia Rais Nicolas Maduro wa Venezuela, lakini Marekani ikatangaza kuweka vikwazo vipya dhidi ya taifa hilo la Amerika Kusini.
Siku moja baada ya Urusi na China kupiga kura ya turufu dhidi ya azimio la Marekani na Ulaya katika baraza la Usalama la Umoja wa mataifa ambalo lilitaka kufikishwa misaada bila vizuizi, Marekani ilisema inawalenga maofisa sita wa jeshi la Venezuela kwa kuzuia msafara ulioongozwa na Marekani mwishoni mwa wiki iliyopita.
Watu wanne waliuawa katika vurumai iliyotokea wakati majeshi ya Maduro yalipozuia tani 178 za mchele, maharage na vyakula vingine kutoka Marekani kuingia nchini humo kupitia Colombia. Kiongozi huyo wa Venezuela amesema msaada huo ni njama za uvamizi zinazoongozwa na Marekani.
“Tunaweka vikwazo dhidi ya wanajeshi wa jeshi la usalama la Maduro kujibu ghasia za ukandamizaji, vifo pamoja na hatua ya kuchoma moto vyakula na madawa vilivyokuwa vinapelekwa kwa wagonjwa na wale ambao hawana chakula nchini Venezuela,” amesema Waziri wa Fedha, Steven Mnuchin, alipowasilisha taarifa ya Serikali kuhusiana na jambo hilo.
Taarifa zinasema kuwa wanajeshi sita waliowekewa vikwazo ni pamoja na Meja Jenerali Richard Jesus Lopez Vargas, Kamanda wa Jeshi la Ulinzi la Taifa. Vikwazo hivyo vinazuia mali zozote zilizoko nchini Marekani na kutoa adhabu kwa shughuli zote za kifedha nchini Marekani zitakazofanywa na maofisa hao.
Marekani pia imeondoa visa kwa maofisa 49 wa Venezuela pamoja na familia zao, wizara ya mambo ya kigeni imesema.
Kiongozi wa upinzani wa Venezuela, Juan Guaido, ambaye Marekani inamtambua kuwa rais wa mpito, alikuwa na matarajio ya kuweza kuingiza shehena ya misaada nchini Venezuela, ambayo Marekani imeratibu pamoja na Colombia na Brazil.
Guaido amesema watu 300,000 huenda wakafa njaa bila ya kuingizwa misaada nchini Venezuela. Umoja wa mataifa unasema Wavenezuela milioni 2.7 wameikimbia nchi hiyo tangu mwaka 2015 wakati taifa hilo lenye uchumi wa kisoshalisti ulipoporomoka, kutokana na kupungua kwa mahitaji muhimu kwa watu.