24.7 C
Dar es Salaam
Tuesday, March 19, 2024

Contact us: [email protected]

Maofisa madini watakiwa kuwa wabunifu

Greyson Mwase-Lindi

MAOFISA madini wakazi wa mikoa nchini, wametakiwa kuongeza ubunifu kwenye ukusanyaji wa mapato ili kuweza kufikia lengo lililowekwa na Serikali, hivyo Sekta ya Madini kuwa na mchango mkubwa kwenye ukuaji wa uchumi wa nchi.

Kauli hiyo imetolewa hivi karibuni na Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo, kwenye kikao na watumishi wa Ofisi ya Ofisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Lindi, wilayani Nachingwea ikiwa ni sehemu ya ziara yake ya siku mbili kwenye mkoa huo, yenye lengo la kukagua shughuli za uchimbaji wa madini pamoja na kutatua kero mbalimbali.

Naibu Waziri Nyongo aliyekuwa ameambatana na Mkuu wa Wilaya ya Nachingwea, Rukia Mhango, alisema Serikali kupitia Wizara ya Madini imeweka mikakati mbalimbali ya kuhakikisha kuwa Sekta ya Madini inakuwa namchango mkubwa kwenye ukuaji wa sekta nyingine kutokana na makusanyo ya kodimbalimbali za madini.

“Ninawaagiza maofisa madini wakazi kuhakikisha wanafikia lengo lililowekwa na Serikali kwenye ukusanyaji wa kodi mbalimbali zitokanazo na Sekta ya Madini kwa kuwa wabunifu na tupo tayari kusaidia pale itakapowezekana,” alisema Nyongo.

Katika hatua nyingine, Nyongo aliwataka maofisa madini kujiridhisha na maeneo yanayoombewa leseni kabla ya kutoa leseni ili kuepusha migogoro inayoweza kujitokeza kati ya wamiliki wa leseni na wananchi wanaozunguka maeneo ya uchimbaji.

Wakati huo huo akizungumza baada ya kuhitimisha ziara yake kwenye kiwanda cha uzalishaji wa saruji cha Dangote kilichopo mkoani Mtwara, Naibu Waziri Nyongo, alisema Serikali kupitia Wizara ya Madini imeweka mazingira mazuri ya uwekezaji kwenye sekta ya madini na kusisitiza kuwa Serikali ipo tayari kutoa ushirikiano kwa wawekezaji ili waweze kuzalisha zaidi na Serikali kupata mapato yake stahiki.

Naibu Waziri alifanya ziara katika machimbo ya kokoto yanayomilikiwa na Kampuni za Drumax Construction na Said Seff na kiwanda cha kutengeneza vyombo vya ibada kwa kutumia madini ya mawe kinachomilikiwa na Shirika la Benedictine Abbey katika Wilaya ya Masasi na kuwahakikishia watendaji wake kuwa Serikali imejipanga katika kutatua changamoto.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
584,000SubscribersSubscribe

Latest Articles