30.2 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Man United yataka bilioni 232 kumuachia Lukaku

 SINGAPORE, Malaysia

 KLABU ya Manchester United imekataa kitita cha Euro milioni  54 (sawa na zaidi ya bilioni 139 za Tanzania) kutoka Inter Milan, kwa ajili ya mshambulaji wao, Romelu Lukaku.

Licha ya ofa hiyo kuwa na kipengele cha kuongezeka, lakin United iliikataa na kutaka kitita cha Euro milioni 90 (sawa na zaidi ya bilioni 232 za Tanzania ) kama walivyomnunua kutoka Everton miaka miwili iliyopita.

 Man United,  ilimnunua Lukaku kwa ada uhamisho wa Pauni milioni 75 (ambazo ni sawa Euro milioni 90).

Lukaku ameachwa nje ya kikosi hicho, kutokana na majeraha, hivyo kukosa michezo mingine miwili ya kujipima nguvu ya awali ambayo United ilicheza ikiwa nchini Australia kabla ya kwenda Singapore.

Hivi karibuni, kocha wa Inter Milan, Antonio Conte alithibitisha kuwa, Lukaku ni muhimu katika mipango yake ya  kuelekea msimu mpya wa Ligi Kuu Italia maarufu Seria A.

Conte alizidiwa mbio na United  katika harakati za kumnasa mshambulaji huyo, wakati akikinoa kikosi cha Chelsea mwaka 2017, ameshindwa kuwa na subira baada ya Inter kushindwa kumsajili Mbelgiji huyo katika kipindi hiki cha majira ya joto

 Kocha huyo raia wa Italia,  tayari ameshamwambia mshambuliaji tegemeo wa kikosi hicho, Mauro Icardi kwamba hatakuwa sehemu ya mipango yake ya msimu ujao, hivyo mabosi wa Inter wafanye haraka kukamilisha usajili wa  Lukaku,

“Lukaku ni mchezaji wa United na haina mjadala, wanajua  vizuri sana kwamba mimi nampenda mchezaji huyo, pia katika siku za nyuma wakati nikiwa kocha wa Chelsea nilijaribu kumsaini.

“Nadhani wakati huu ikiwa unasema kuhusu mchezaji kutoka klabu nyingine ni haki ya kuzungumza juu ya Lukaku kwa sababu tuna heshima kubwa kwa United.

“Kama nilivyosema hapo awali, nampenda mchezaji huyu na kumwona kuwa mchezaji muhimu kwa sisi kuwa na uboreshaji mzuri, lakini wakati huo huo kuna soko la uhamisho.

“Tunajua vizuri hali yetu kwa sasa na tutaona kinachotokea, lakini kwa sasa Lukaku ni mchezaji wa United.

“Si rahisi kucheza dhidi ya timu kama Juventus na Manchester United bila mshambuliaji mahiri, lakini soko liko  wazi hivyo bado tutajitajidi kusajili wachezaji na kuwaachia wengine,”alisema Conte.

Kocha wa United, Ole Gunnar Solskjaer, alikiri kwamba Lukaku atapoteza mchezo wake wa tatu mfululizo kwenye ziara yao, baada miwili iliyotangulia dhidi ya  dhidi ya Perth Glory na Leeds United.

 “Hapana, hayupo fiti hivyo hawezi kuwapo, sina taarifa yoyote tangu nilivyozungumza nae mara ya mwisho.

 “Luka (Shaw) amekosa siku kadhaa, Anthony (Martial) siku moja na Romelu ndiye aliyekosa siku zote,” alisema Solskjaer.

 Lukaku ameonyesha nia ya kutaka kuihama klabu hiyo msimu huu ili akatafute changamoto nyingine.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles