25.2 C
Dar es Salaam
Tuesday, April 23, 2024

Contact us: [email protected]

MAMBO MATANO YA KUFANYA BAADA YA KUHITIMU CHUO

wahitimu-wa-chuo-cha-elimu-ya-biashara-cbe-wakati-wa-mahafali-yaliyofanyika-chuoni-hapo-hivi-karibuni
wahitimu-wa-chuo-cha-elimu-ya-biashara-cbe-wakati-wa-mahafali-yaliyofanyika-chuoni-hapo-hivi-karibuni

Na JONAS MUSHI


WAKATI tukishuhudia maafali ya vyuo vingi mwishoni mwa mwaka huu ni wazi kwambaTanzania inaendelea kuvuna rasilimali watu yenye maarifa na ujuzi wa kupambana na changamoto mbalimbali za maisha ya mwanadamu.

Tanzania bado ni nchi inayosumbuliwa na umaskini na changamoto za maendeleo na ustawi wa jamii ni nyingi ukilinganisha na nchi zilizoendelea. Elimu inatajwa kuwa njenzo muhimu ya kuondokana na umaskini kwani huipa jamii mbinu za kupambana na changamoto za maisha.

Takwimu zinaonyesha hapa nchini kuna watu zaidi ya 100,000 wanaoingia kwenye soko la ajira kila mwaka.

Hata hivyo wanaofanikiwa kuingia katika ajira rasmi ni asilimia ndogo ukilinganishwa na wanaobaki bila ajira rasmi.

Katika makala haya tutaangalia mambo matano muhimu ya kufanya baada ya kuhitimu chuo ukiwa bado hujapata ajira au kuanza kazi yeyote.

  1. Kutana na watu waliokutangulia wenye mafanikio

Wahitimu wengi huwa wanafikiria kupata maendeleo baada ya kazi na kuwa kama fulani lakini wanakuwa hawajui mtu huyo alianzaje na alifanikiwa vipi.

Baada ya kuhitimu ni muda mzuri wa kuwatembelea watu wenye mafanikio na kuzungumza nao, epuka kutumia muda mwingi kukaa na watu ambao hawana tofauti na wewe kimaendeleo. Tumia muda mwingi kukaa na watu ambao unataka uwe kama wao.

Hii itasaidia kukuondolea upweke wakati ukiwa hujapata kazi na kukupa njia ya kufikia malengo yako kwa kujifunza kwa waliofanikiwa.

  1. Jiwekee utamaduni wa kuandika miradi inayohusu taaluma yako

Unapomaliza masomo ya darasani lazima utambue kuwa kile ulichojifunza huu ndio wakati wa kukifanyia kazi. Tumia muda wako kubuni miradi unayoweza kuifanya ukiwa umeajiriwa au kujiajiri.

Hii itakusaidia kujiandaa vizuri zaidi katika kuingia kwenye soko la ajira ambalo linahitaji watu wenye mawazo mapya ya kupambana na changamoto zilizopo kwenye taaluma husika.

Tambua kuwa changamoto huwa haziishi hivyo lazima kufikiria nyuma ya ulimwengu unaoishi kuweza kugundua namna bora zaidi ya kufanya kile kilichopo sasa kiweze kuwa na matokeo mazuri zaidi.

Hii itakufanya uwe mtafutaji kazi mzuri zaidi ambaye anajua kile anachoenda kukifanya. Waajiri wengi sasa hivi wanataka watu ambao wana kitu kipya cha kufanya kwenye kampuni zao kuliko wale wa kwenda kuambiwa cha kufanya.

  1. Tafuta kazi za kujitolea

Kabla hujaanza kufikiria kuajiriwa ni vyema ukaanza kufikiria kujitolea. Wahitimu wengi huputa msongo wa mawazo pale wanapoanza kufikiria kupata ajira baada ya kuhitimu. Wengine huenda mbali zaidi na kuanza kufikiria kupata mshahara mkubwa.

Ni vizuri kuwa na malengo hayo lakini ukawa na fikra za kuanza chini. Unapokuwa unajitolea ndio fursa ya kumshawishi mwajiri kwamba wewe ni mtu muhimu katika kampuni yake kwahiyo muda wote unapofanya kazi unafanya kama upo kwenye usaili kwa bidii ya kuonyesha umuhimu wako.

Lakini hii itakusaidia kukuondolea upweke na msongo wa mawazo pia itakupa fursa ya kukutana na watu wengi ambao wanaweza kukusaidia katika kuona firsa zingine.

  1. Ishi maisha yako

Watu wengi hupenda kujilinganisha na wenzao wenye sifa zinazofanana, mfano umri na kiwango cha elimu na kutaka waishi maisha yanayofanana. Tabia hii si nzuri kwa sababu inaweza kuleta wivu mbaya na kukuongezea msongo wa mawazo na kukufanya ukate tamaa.

Unaweza kumwona mwenzako wa sifa zako ameanza kuishi maisha ya kujitegemea na wewe ukawa unatamani kufanya hivyo lakini huna uwezo au uwezo wako ni mdogo na ikakupa msongo wa mawazo.

Usidanganyike kuishi na wazazi hakukufanyi uonekane bado mtoto cha msingi ni kujishughulisha, acha kukaa bure kile kidogo unachopata saidia nyumbani na hakikisha unajifanyia usafi kwa kutunza chumba chako mwenyewe na kufua nguo zako badala ya kuwapa wazazi wako au msaidizi wa nyumbani.

Hakikisha unakuwa na malengo ya muda wa kukaa nyumbani na ukitoka unataka ukaishi vipi na wapi.

  1. Acha tamaa za utajiri wa haraka

Usidanganyike kwamba kuwa na stashahada au shahada ndio kuanza kupata fedha nyingi na kuishi maisha mazuri. Si kweli kumbuka elimu uliyopata ni ya kusaidia kutatua changamoto ya jamii yako. Sasa hivi wapo watu wanaohitimu elimu za juu na kutokana na shauku ya kuwa na maisha mazuri hujikuta wakijiingiza kwenye vitendo viovu kusaka utajiri wa haraka kama vile kuuza dawa za kulevya na kuiba fedha kwa njia ya mtandao.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles