24.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

MAKONDA AMUOMBA JPM AWAPE JWTZ MRADI WA NSSF

MWANDISHI WETU -DAR ES SALAAM

MKUU wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, amemuomba Rais Dk. John Magufuli kuwapatia JWTZ mradi wa ujenzi wa Nyumba za NSSF zilizopo Kata ya Toangoma ambazo ujenzi wake umesuasua zaidi ya miaka 15, jambo linaloisababishia serikali hasara.

Makonda amesema anaamini kwa utendaji kazi wa vijana wa JWTZ, utawezesha majengo hayo kukamilika ndani ya muda mfupi na kuanza kutumiwa.

Hatua hiyo imekuja baada ya Makonda kuendelea na ziara ya ukaguzi wa miradi ya maendeleo, ambapo jana ilikuwa zamu ya ukaguzi wa maendeleo ya ujenzi wa majengo 12 ya magereza Ukonga, ambayo hivi karibuni Rais Magufuli aliwanyang’anya Wakala wa Majengo nchini (TBA) baada ya kusuasua na kuwakabidhi JWTZ, ambapo sasa ujenzi unakwenda vizuri.

Kutokana na hayo, Makonda pia amewapongeza JWTZ kwa kasi kubwa wanayoonyesha katika mradi huo na kueleza kuwa anaamini watakamilisha ujenzi ndani ya muda uliokusudiwa.

Kwa upande wa msimamizi wa ujenzi huo, Brigedia Charles Mbuge, amesema ujenzi wa majengo hayo utakamilika na kukabidhiwa ndani ya miezi miwili na nusu.

Wakati huo huo, Makonda ameshangazwa na malipo makubwa yanayofanywa katika miradi ya DMDP, akiwataka  Takukuru kuanza uchunguzi mara moja.

Amemwagiza Mkurugenzi wa  Takukuru Mkoa wa Dar es Salaam kufanya uchunguzi wa utaratibu wa upatikanaji wa  tenda kwenye miradi ya DMDP. 

“Haiwezekani kilomita moja ya barabara ya DMDP Wilaya ya Kinondoni inajengwa kwa shilingi bilioni 2.7, wakati kwa Wilaya ya Temeke barabara kama hiyo inajengwa kwa shilingi milioni 900,” alisema.

Makonda amebaini madudu hayo wakati wa mwendelezo wa ziara yake ya ukaguzi wa miradi ya maendeleo kupitia fedha zinazotoka Serikali Kuu, Halmashauri na fedha za wahisani, ambapo amekwazwa na matumizi mabaya ya fedha za mkopo kutoka Benki ya Dunia.

“Barabara za DMDP zimekuwa zikijengwa kwa kiasi kikubwa cha pesa kuliko zile za Tanroads ambazo kwanza zina ubora mkubwa, uwezo wa kubeba mzigo mkubwa na pia ni pana, katika miradi ya ujenzi wa barabara, hospitali na shule nawapongeza Manispaa ya Temeke kwa kazi nzuri na kusimamia vizuri miradi ya maendeleo, niwaombe muongeze bidii na kasi,” alisema Makonda.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles