24.5 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

MAKAPU ABEBA MAJUKUMU YA TSHISHIMBI YANGA

Na THERESIA GASPER-DAR ES SALAAM

KOCHA wa Yanga, George Lwandamina, anatarajia kumtumia kiungo, Said Makapu, kama mbadala wa Papy Tshishimbi, wakati timu hiyo itakapoivaa Mtibwa Sugar kesho.

Pambano hilo la Ligi Kuu Tanzania Bara kati ya Yanga na Mtibwa litapigwa kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam.

Katika mchezo huo, Yanga itakosa huduma ya Tshishimbi ambaye atakuwa anatumikia adhabu ya kukosa mchezo mmoja kutokana na kuwa na kadi tatu za njano.

Hiyo itakuwa mara ya kwanza kwa Makapu kucheza pambano la Ligi Kuu msimu huu kama Makapu atapata fursa ya kuivaa Mtibwa kesho.

Kiungo huyo raia wa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo (DRC), amekuwa nguzo muhimu ya Yanga akitumika kama kiungo mkabaji tangu alipojiunga wakati wa dirisha la usajili la msimu huu akitokea Mbambane Swallows ya nchini Swaziland.

Katika mazoezi yaliyofanyika jana Uwanja wa Uhuru, Lwandamina alimpanga Makapu akigawa vikosi viwili, huku Makapu akitupwa kile kilichojumuisha nyota muhimu wa timu hiyo ambao wamekuwa wakianza katika mechi mbalimbali.

Kikosi kilichoonekana cha kwanza kwa kuangalia mechi za timu hiyo zilizopita kilikuwa na Donald Ngoma, Ibrahim Ajib, Obrey Chirwa, Juma Makapu, Raphael Daud, Juma Abdul, Makapu, Pius Buswita, Juma Abdul, Andrew Vincent ‘Dante’, Kelvin Yondani na Beno Kakolanya.

Kingine kiliundwa na Matheo Antony, Emmanuel Martin, Baruan Akilimali, Pato Ngonyani, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Juma Mahadhi, Yusuph Mhilu,  Tshishimbi, Mwinyi Haji, Abdallah Shaibu ‘Ninja’ na Ramadhani Kabwili.

Vikosi hivyo vilicheza bonge la mechi, ambapo kile cha akina Makapu kiliibuka na ushindi wa mabao 2-0 yaliyowekwa wavuni na Ajib.

Yanga inakamata nafasi ya sita kwenye msimamo wa Ligi Kuu, ikiwa imejikusanyia pointi nane sawa na timu za Simba na Singida United, lakini zikitofautiana kwa idadi ya mabao ya kufunga na kufungwa.

Imevuna pointi hizo baada ya kushuka dimbani mara nne na kufanikiwa kushinda mechi mbili na kutoka sare mbili.

Mtibwa itakayoumana na Yanga kesho inakamata usukani wa ligi hiyo ikiwa na pointi 10, ilizozipata baada ya kushinda  michezo mitatu na sare moja.

 

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles