25.2 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Makamba adaiwa kuasisi rushwa ndani ya CCM

Yusuph MakambaNa Kulwa Mzee, Dar es Salaam

KATIBU Mkuu wa zamani wa CCM, Yusuph Makamba amedaiwa ndiye aliyeasisi  rushwa ndani ya chama hicho.

Hayo yalielezwa  na mwanachama wa Chadema, Hamisi Mgeja, ambaye aliwahi kuwa Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Shinyanga.

Mgeja alikuwa akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana.

Alisema Makamba aliupotosha umma alipokuwa katika Mkutano Mkuu Maalum wa CCM uliofanyika Dodoma wiki chache zilizopita aliposema kuwa Rais Mstaafu Jakaya Kikwete alimuacha Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa katika kinyang’anyiro cha urais kwa sababu ya ufisadi.

“Napinga, hiyo si sababu ya kweli. Makamba alipokuwa KatibuMkuu  hakuna kikao hata kimoja kilichowahi kusema Lowassa ni fisadi. Hata alipotaka kugombea urais kupitia Chadema hakukuwa na pingamizi juu yake.

“Nyota ya Lowassa iliyong’aa ndiyo iliyomgharimu… Makamba hawezi kusimama kuwasema wengine.

“Yeye ndiye mwasisi wa rushwa ndani ya CCM.  Alikuwa akiita (akiikaribisha) rushwa baada ya kupokea kijiti kutoka kwa Philip Mangula,”alisema.

Alidai  Makamba aliyewahi kuwa Mkuu wa Wilaya ya Kibondo anajua alifukuzwa kwa sababu zipi.

“Naomba Watanzania wampuuze. Makamba ni kama nyoka asiye na sumu, anazeeka vibaya.  Alipokuwa Katibu Mkuu CCM  alikuwa jipu lililoshindwa kupasuka mpaka alipostaafu.

“Alipokuwa mtendaji mkuu ndani ya CCM rushwa iliota mizizi… hana usafi wa kuwasema wengine ni vema akajitathimini ikiwezekana akaye kimya   kulinda heshima yake,”alisema Mgeja.

Makamba alipotafutwa na Mtanzania kuzungumzia tuhuma zilizoelekezwa kwake, alisema hana muda wa kubishana.

“Sina muda wa kubishana na wajinga, wapumbavu… ukibishana na mpumbavu nawe utaonekana mpumbavu, watu hawataona tofauti.

“Narudia tena mama, sina muda wa kubishana na wapumbavu, ukibishana, nawe utaonekana mpumbavu, tofauti haitaonekana,”alisisitiza.

Akizungumzia kauli ya Rais John Magufuli alipokuwa Dodoma kwamba angekuwa Rais Kikwete   wote waliomshangilia Lowassa ukumbini angewapoteza, Mgeja  alisema uwezo huo hana.

Alisema inawekana hata Rais Kikwete alikasirika zaidi yake lakini hakuwa na uwezo wa kufanya lolote.

Alimshauri  asome Ibara ya 107 ya Katiba ya CCM  imwongoze mipaka yake.

“Lugha aliyotumia ilikuwa ya kujenga hofu, hao ambao angewamaliza asilimia 85 wamo ndani ya CCM na ndiyo atakaofanya nao kazi kwa sababu  miongoni mwa waliomtaja Lowassa wako mawaziri wake,”alisema.

Alisema hakuna mwenye uwezo wa kumjaribu Rais bali wanapopashana habari za  siasa anatakiwa kuwa mvumilivu.

“Anasema vyama vimechoka, hakuna chama kilichochoka…kama mwanasiasa mwenzetu anatakiwa kutumia lugha ya ustaarabu.

“Iliyopita mwaka 2015 ilikuwa mvua ya rasharasha, masika yanakuja mwaka 2020.  Asivibeze vyama vya siasa, aviheshimu, sote tuna haki,”alisema.

Mgeja alisema wanaohama Chadema kurudi CCM wanahama kwa matakwa yao.

Alisema  yeye na wenzake wanapata ushirikiano mzuri huko waliko.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles