33.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

MAJALIWA MGENI RASMI SIMBA DAY

  • Mastaa wa Bongo Fleva, Bongo Movie kupamba tamasha

NA WINFRIDA MTOI


WAZIRI Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa, anatarajia kuwa mgeni rasmi katika tamasha la Siku ya Simba ‘Simba Day’, litakalofanyika Agosti 8, mwaka huu, Uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam.

Katika tamasha hilo, Wekundu wa Msimbazi,  Simba, watashuka dimbani kuumana na Asante Kotoko ya Ghana.

Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano ya Simba, Haji Manara, alisema mbali ya pambano hilo, pia kutakuwa na burudani kutoka kwa wasanii wa muziki wa Bongo Fleva na filamu wanaounda umoja unaofahamika kama ‘Bongo Movie.’

Aliwataja wasanii hao kuwa ni Yvonne Cherly ‘Monalisa,’ Jacob Steven `JB`, Idris Sultan, Anti Ezekiel kwa upande wa Bongo Movie, wakati  Vanessa Mdee, Mwasiti, Msaga Sumu na bendi ya Twanga Pepeta itawakilisha wasanii wa muziki.

Manara alisema mwaka huu wamepania kulifanya tamasha hilo kuwa la tofauti na ambayo yamekuwa yakifanyika miaka ya nyuma, kwa kuwa watakuwa wanaadhimisha wakiwa ni mabingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara, baada ya kuukosa kwa miaka sita.

“Kwa Wanasimba, safari hii sio ya kukosa kufika uwanjani, itakuwa ni nafasi pia ya kuwaona wachezaji wapya waliosajiliwa, kama vile Mzambia Clotous Chama na vitu vya kocha mpya Mbelgiji Patrick Aussems,” alisema Manara.

Manara alisema maadhimisho ya Simba Day yalianza tangu jana, ambapo mchezaji wao mkongwe, Abdallah Kibadeni, alimtembelea mkongwe mwenzake, Sunday Manara.

Alisema pia watafanya usafi na kuchangia damu  hospitalini kabla ya  Agosti 8.

Pia kikosi chao kilichopo kambini nchini Uturuki  kinatarajia kurejea nchini Jumatatu kabla ya Jumanne kwenda kutoa msaada katika kituo cha watoto yatima kilichopo Kawe, jijini Dar es Salaam.

Wakati huo huo, mchezo wa kirafiki kati ya   Simba na Tanger Ettihad uliopangwa kufanyika jana jioni uliahirishwa kutokana na mvua kubwa na kusababisha Uwanja wa Hotel ya The Green Park, Kartepe jijini Instanbul, Uturuki kujaa maji.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles