31.7 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

MAHAKAMA ZITENDE HAKI, ZIONDOE MASWALI

TUMEPATA kuandika huko nyuma, na leo tunarudia tena juu ya umuhimu wa kila mtu katika eneo lake kuhakikisha anatenda haki.

Tumekuwa tukisisitiza hilo kwa sababu pale haki inapodhulumiwa, matokeo yake huwa si mazuri, kwa mfano tutajikuta tumezalisha chuki, mifarakano, visasi n.k.

Tuliwahi kuandika huko nyuma na kusisitiza kwamba, kila mtu na hasa ile mihimili mitatu, kwa maana ya Serikali, Bunge na Mahakama, ambayo kimsingi imepewa nguvu ya kimamlaka, kwamba inapaswa kutambua kuwa, wajibu wao ni kutafuta namna ya kutatua matatizo na si kuyaongeza.

Kwa mfano, mhimili ambao umekuwa ukijadiliwa na kunyooshewa kidole mara kwa mara ni Mahakama, licha ya viongozi wake kuchukua hatua mara kwa mara ya kurekebisha utendaji wake wa ndani.

Mara nyingi huwa haipiti mwezi au miezi pasipo mhimili huo kunyooshewa vidole, kwani leo hii kuna malalamiko kuwa, wapo mahabusu ambao wana haki ya kupata dhamana, lakini wamenyimwa.

Si hivyo tu, pia inaelezwa lipo kundi la mahabusu ambalo liko ndani kwa muda mrefu kwa sababu tu ya upelelezi  kuchukua muda mrefu kukamilika au Mahakama ambayo kesi hiyo imefikishwa kudai kuwa, haina uwezo nayo, hivyo kusubiri taratibu fulani fulani.

Wataalamu wa sheria wanasema sheria zipo wazi kuhusu kumfikisha mtu Mahakamani na muda wa upelelezi kukamilika, lakini mara kadhaa hali imekuwa ni tofauti.

Wanasema lugha hiyo imekuwa ikileta mkanganyiko kwa jamii na hivyo kuzua tafsiri tofauti tofauti, ikiwamo kuiona Mahakama kama chombo ambacho pengine hakitoi sura iliyobeba lengo la kuanzishwa kwake.

Kwa sababu hiyo, Mahakama inaonekana kubeba taswira tofauti kabisa.

Mambo haya yanasemwa kila wakati na kwa bahati nzuri tulipata kuandika kuwa, zipo ripoti ambazo zinaonyesha kuwa, barani Afrika kwa muda mrefu sasa watu wameumizwa na vitendo vya kudhulumiwa haki zao za msingi.

Kwa mujibu wa ripoti hizo, hata kutopea katika umaskini wa kimawazo, na hivyo wengi kuhadaika na kauli za wanasiasa, viongozi na watu wenye nafasi katika jamii, msingi wake ni dhuluma ya haki zao za msingi.

Kwa misingi vyombo vilivyopewa mamlaka kikatiba vinao wajibu mkubwa wa kuchunguza, kusikiliza, kubadilisha na kuboresha ili kupunguza matatizo yanayoikabili jamii.

Vyombo hivi vinapaswa kutambua kwamba, chochote kitakachofanyika bila kufuata misingi ya kutenda haki kitakwenda kuathiri mustakabali mwema wa Taifa letu.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles