23.8 C
Dar es Salaam
Thursday, April 25, 2024

Contact us: [email protected]

Mahakama za kimila ‘Dagashida’ zatesa walimu  

Na SAMWEL MWANGA – SIMIYU

MAHAKAMA za kimila, maarufu kwa jina la Dagashida, zinazoendeshwa na wazee wa kimila maeneo ya vijijini mkoani Simiyu, zimeendelea kuwa mwiba mkali kwa wafanyakazi, hasa walimu  kutokana na kuchapwa viboko hadharani.

Mfumo wa Dagashida umekuwa ukitumiwa na viongozi wa kimila katika maeneo mengi mkoani Simiyu kuadhibu wananchi, hususani watumishi wa umma, kwa kuwalipisha faini ya fedha, mazao, wanyama na kuchapwa viboko pale wanapoonekana kwenda kinyume na matakwa yao ya kimila, ingawa wakati mwingine wamekuwa wakizushiwa.

Mbali na walimu, wafanyakazi wengine ambao wameendelea kuonja joto la mahakama hizo ni wafanyakazi wa Idara ya Afya katika zahanati na

vituo vya afya, watendaji wa vijiji pamoja na kata.

Mahakama hizo, zinadaiwa kutoa adhabu kali kwa wafanyakazi hao, ikiwemo kuchapwa viboko mbele ya wananchi na wanafunzi, kutengwa pamoja na kutozwa faini kubwa kwa makosa mbalimbali wanayokutwa nayo watuhumiwa.

Kutokana na mahakama hiyo kuendelea kujichukulia sheria mkononi, imeanza kuathiri mno watumishi wa Serikali wanaopangiwa kufanya kazi mkoani Simiyu.

Wengi wao wameanza kukataa kwenda kwenye vituo vya kazi mkoani humo kwa madai kuwa wamekuwa wakidhalilishwa na kuvunjiwa utu wao mbele ya jamii inayowazunguka.

Kaimu Katibu wa Chama cha Walimu Tanzania (CWT), Wilaya ya Bariadi, Baraka Owawa, alisema kuwa wamekuwa wakipokea kesi nyingi za walimu kuchapwa viboko hadharani.

Alisema hali hiyo imewafanya wakate tamaa kufanya kazi maeneo mbalimbali wanayopangiwa.

“Kesi za mfano ziko Wilaya ya Itilima na Meatu, walimu wamechapwa dagashida mbele ya hadhara… wanachapwa fimbo kama

watoto, wengine wametengwa, huku baadhi yao wamekuwa wakitozwa faini kubwa kama ng’ombe mmoja kwa kosa,” alisema Owawa.

Baada ya kushamiri manyanyaso hayo, Serikali imeamua kupiga marufuku uendeshaji wa mahakama hizo kwa madai zinadhalilisha utu wa mtu pamoja na kuwa ni mila zilizopitwa na wakati ambazo hazina faida kwa jamii.

Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Anthony Mtaka, alisema tabia ya viongozi wa kimila kuwaadhibu wananchi na watumishi wa umma wanaokutwa na  makosa, haikubaliki hata kidogo.

Aliwataka wakuu wa wilaya ambao ni wenyeviti wa kamati za ulinzi na usalama, kulisimamia

suala hilo na kuwakamata wahusika wote.

“Wakuu wa wilaya ni wenyeviti wa kamati za ulinzi na usalama, kasimamieni suala hili na mhakikishe linakomeshwa. Sitaki kusikia kitu kinachoitwa dagashida. Hatuwezi kuacha wananchi wanateseka, watumishi wetu tunaowaleta kuwatumikia wananchi nao wanateseka na mifumo kandamizi kama hii wakati vyombo vyetu vya ulinzi na usalama vipo,” alisema Mtaka.

Alisema kuna wazee wa kimila ‘Sumbantale’ ambao wanapaswa kudhibitiwa au kukamatwa na kupelekwa polisi ili wachukuliwe hatua za kisheria.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles