28.2 C
Dar es Salaam
Saturday, April 20, 2024

Contact us: [email protected]

MAGUFULI NI SAHIHI KUMZIMA MWAKYEMBE

JUZI ilitangazwa na vyombo mbalimbali vya habari kuwa Serikali imepiga marufuku ufungishaji ndoa za aina zote, iwe za kidini, kimila na kiserikali bila kuwa na cheti cha kuzaliwa kinachotolewa na Wakala wa Usajili, Ufilisi na Udhamini (RITA) kuanzia Mei mosi, mwaka huu.

Kauli hiyo ya Serikali ilitolewa na Waziri wa Katiba na Sheria, Dk. Harrison Mwakyembe, wakati akiwa katika ziara yake mkoani Morogoro.

Dk. Mwakyembe alisema Serikali imeamua kufanya hivyo ili kuwa na takwimu sahihi za wananchi wake iweze kupanga mipango ya kimaendeleo sambamba na kuzuia wageni kuingia kinyemela nchini.

Dk. Mwakyembe aliitaka RITA kuhakikisha inasimamia sheria ya usajili kwa sababu bila nchi kuwa na takwimu sahihi za  vizazi na vifo au ndoa, inasababisha ishindwe kusonga mbele kimaendeleo.

Kwamba ndiyo maana nchi zilizoendelea zinatoa kipaumbele katika suala zima la usajili kwa wananchi wake.

Alisema wenzetu katika nchi zilizoendelea, suala la usajili wamelipa kipaumbele wakati sisi bado tuko nyuma, na akasisitiza lazima tubadilike kuanzia Mei, mwaka huu.

Akitoa mfano kwa  Mkoa wa Morogoro, alisema kwa mujibu wa sensa ya watu na

makazi ya mwaka 2012, mkoa huo una wakazi milioni 2.2,

lakini waliosajiliwa na kuwa na vyeti vya kuzaliwa ni asilimia 11 tu.

Wakati Watanzania wakiwa wanaishangaa amri ya Dk. Mwakyembe ambayo ilikuwa haieleweki na wala haionyeshi jinsi ambavyo RITA  itahakikisha na kusimamia sheria ya usajili ili Serikali iwe na takwimu sahihi za wananchi wake iweze kupanga mipango ya kimaendeleo sambamba na kuzuia wageni kuingia kinyemela nchini, Rais Dk. John Magufuli akawapa ahueni.

Rais ameifuta amri ya Dk. Mwakyembe iliyokuwa inatoa sharti la kuwa na cheti cha kuzaliwa watu wote watakaofunga ndoa kuanzia mei 1, mwaka huu.

Kwamba serikali haiwezi kuruhusu sharti hilo kutumika kwa kuwa litawanyima haki Watanzania wengi kuoa au kuolewa ambao hawana vyeti vya kuzaliwa, huku utaratibu wa kupata vyeti hivyo ukiwa na changamoto nyingi kwa wanaohitaji, na hasa wale wa vijijini.

Kwamba Watanzania walio na vyeti vya kuzaliwa ni chini ya asilimia 20 huku wengi wao wakiwa ni wale waishio vjijini ambako ni vigumu kupata vyeti hivyo, na wengine wakiwa walizaliwa kabla ya kuanza kutolewa kwa vyeti vya kuzaliwa nchini mwaka 1961.

Rais Dk. Magufuli kwa kuona matatizo yanayoweza kuwapata Watanzania baadaye, pia ametoa wito kwa wanasheria kuziangalia vizuri sheria zinazohusiana na kuzaliwa na vifo  hali kadhalika kuoa na kuolewa ili zisilete mkanganyiko kwa wananchi.

Zaidi akiwahimiza Watanzania kuendelea kupata vyeti vya kuzaliwa kama kawaida, na kwamba viongozi waendelee kuwahamasisha wananchi kuwa navyo.

Tunasema Rais Dk. Magufuli amefanya jambo la maana kwa kumbana haraka Dk. Mwakyembe asilete taharuki kwenye jamii kwa kutoa kauli zisizo na uhalisia.

Tunatoa rai kuwa Serikali iwe na utaratibu wa kutoa matamko ya kutekeleza badala ya kiongozi yeyote kutoa amri zinazojenga hisia za kuwako kwa  ila kama alivyofanya Dk. Mwakyembe.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles