Anna Potinus
Rais Dk. John Magufuli amewataka viongozi kutumia fedha zinazotolewa katika ujenzi wa miradi mbalimbali ipasavyo na kuachana na tabia ya kuzitumia vibaya kwa mambo binafsi.
Ameyasema hayo leo Aprili 9, alipokuwa akihutubia wananchi wa mkoa wa Ruvuma na kufunga ziara yake ya siku Tano mkoani humo iliyoanza tangu Aprili 4, ambapo amezindua kituo cha afya cha Madaba na kuwataka wakazi wa mkoa huo kuendelea kudumisha amani na mshikamano kwa maendeleo ya nchi.
Rais Magufuli ametoa wito kwa wakurungenzi kuhakikisha fedha zinazotolewa katika ujenzi wa vituo vya afya na mambo mengine zinatumika ipasavyo na si vinginevyo kwasababu anapenda viongozi wanaosimamia fedha za nchi.
“Fedha sio kwamba zilikuwa haziji ila zikija na kupelekwa kwenye halmashauri zinaliwa tukaona tubadilishe utaratibu fedha ikitolewa inaenda moja kwa moja kwa wananchi katika ujenzi wa hospitali,” amesema.
Aidha amesisitiza umuhimu wa sekta ya afya ambapo amesema kuwa taarifa ya shirika la afya duniani (WHO) inasema kwamba nguvu kazi iliyopotea kutokana na masuala ya afya ni sawa na masaa milioni 630.