30.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Magufuli aigwaya hukumu ya EACJ

Na Mwandishi Wetu, Dar es Salaam

SERIKALI imepatwa na kigugumizi baada ya Mahakama ya Afrika Mashariki (EACJ) iliyoizuia Serikali ya Tanzania kujenga barabara ya lami kupitia Hifadhi ya Taifa ya Serengeti.

Hatua hiyo inaelezwa kuwa ujenzi huo utaathiri mazingira, maisha ya wanyamapori na baoanuai ya hifadhi hiyo.

Akizungumza na MTANZANIA jana mjini Dodoma kuhusu uamuzi huo wa Makahama ya EACJ, Waziri wa Ujenzi Dk. John Magufuli, alisema kwa sasa hawezi kuzungumzia suala hilo la kimahakama.

“Ninakuomba achana na hiyo kitu maana huo ni uamuzi wa mahakama siwezi kusema lolote kwa sasa ninakushukuru kwa kuniuliza,” alijibu Dk. Magufuli kwa kifupi.

Hata hivyo kauli hiyo ya Waziri Magufuli inapingana na ile aliyowahi kuitoa ambapo alisisitiza kuwa Serikali ya Tanzania haitishwi na wanaharakati wa Kenya kwenda kufungua kesi hiyo.

“Hii ni nchi yetu na tutaendelea na utaratibu wa ujenzi wa barabara, haiwezekani maisha ya Watanzania yasiboreshwe kuliko ya wanyama,” alisema Magufuli alipokuwa akitoa misimamo kuhusu ujenzi huo.

Oktoba 6, mwaka 2012 alisema anashangazwa na jitihada za upotoshaji wa makusudi wa ukweli kuhusu miradi ya maendeleo inayobuniwa na kuanzishwa na Serikali yake.

Alisema upotoshaji huo wa makusudi hautaifanya Serikali yake kubadilisha maamuzi yake kuhusu miradi ya maendeleo ya wananchi ama kuacha kubuni miradi mipya zaidi.

“Kamwe hatujapata kuwa na mipango ya kujenga barabara ya lami kukatisha Mbunga ya Serengeti. Huu ni upotoshaji wa kushangaza. Najua ni upotoshaji wa makusudi hata kama sijui unaanzia wapi. Tumesema na kusema tena kuwa tunalo jukumu la maendeleo kwa wananchi wote wakiwemo wa Loliondo na Mugumu ambao tumesema kuwa tutawajengea barabara ya lami,” alisema.

Juni 20, mwaka huu katika hukumu iliyotolewa jijini Arusha, jopo la majaji watatu wa mahakama hiyo wakiongozwa na Jaji Kiongozi Jean Bosco Butasi, liliiamuru Tanzania kutotekeleza mradi wowote wa ujenzi au ukarabati wa barabara hiyo utakaokuwa na madhara kwa mazingira na baoanuai ya hifadhi ya Serengeti.

Hukumu hiyo ilitolewa baada ya Taasisi ya Africa Network For Animal Welfare (ANAW) ya jijini Nairobi, Kenya kufungua kesi dhidi ya Serikali ya Tanzania kupinga ujenzi wa barabara hiyo yenye urefu wa kilomita 239, ikidai itaathiri mazingira, uhai wa wanyama na baoanuai wa Hifadhi ya Serengeti kwa kuongeza shughuli za kibinadamu.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles