Veronica Romwald na Maria Kaira (RCT), Dar es Salaam
MADALALI nane wa kituo cha mabasi yaendayo mkoani cha Ubungo, wamepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Jiji kwa kosa la kuwabughudhi abiria.
Washtakiwa hao ni God Mgunda (38), Godwin Mchao (26), Kasim Salum (27), Mozati Mshauri (20), Winsilaus Mrema (36), Colimba Hamis (36), Sinaa John (27) na Abdallah Tesha (43).
Akisoma shtaka hilo juzi mbele ya Hakimu Mkazi, Timoth Lyon, Mwendesha Mashtaka, Neema Haule alidai washitakiwa hao walitenda kosa hilo Juni 25 mwaka huu kituoni hapo ambapo walikamatwa na Askari, Shaban Kihiyo.
Mshitakiwa namba moja na nane katika shtaka hilo walikubali kutenda kosa na kutakiwa kulipa faini ya Sh 50,000 na kutumikia kifungo cha miezi mitatu jela.
Washtakiwa wengine walikana kutenda kosa hilo na kutakiwa kuwa na wadhamini wawili ambao watatoa kiasi cha Sh 400,000 kama dhamana, kesi hiyo itatajwa tena mahakamani hapo Julai 8, mwaka huu.