25.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Maalim, Dk. Shein wapigana vikumbo Z’bar

Dk. Ali Mohamed Shein na maalim seifNa Mwandishi Wetu, Zanzibar

MAFAHARI wawili waliohasimiana katika siasa tangu ulipomalizika uchaguzi wa marudio Visiwani Zanzibar, Maalim Seif Sharif Hamad na Rais wa Zanzibar, Dk. Ali Mohamed Shein, ni wazi hivi sasa wanapigana vikumbo.

Kupigana  vikumbo huko kumetokea jana wakati Maalim Seif alipokuwa katika ziara yake ya  chama katika Wilaya ya Kaskazini B  Kisiwani Unguja huku Dk. Shein akitua Kisiwani Pemba na kuzungumza na wana CCM wilayani Chakechake.

Dk. Shein, aliwasili Kisiwani Pemba, ikiwa ni siku chache tangu Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif, afanye ziara ya siku nne na kueleza mikakati yake ikiwamo  mgomo na kuindoa madarakani Serikali ya   Dk. Shein ikiwa ni kupinga   uchaguzi wa marudio uliofanyika Macho 20, mwaka huu ambako CCM iliibuka na ushindi.

Ziara hiyo ya  chama kwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.   Shein ni ya kwanza tangu ulipomalizika uchaguzi huo wa marudio ambao CUF iliususa.

Akizungumza na wana CCM jana, Dk. Shein aliwashukuru kwa kufanikisha uchaguzi wa marudio uliofanyika Machi, mwaka huu na kukipa ushindi wa kishindo chama hicho.

“Wana CCM mlionyesha ujasiri mkubwa katika uchaguzi wa marudio hadi kukipatia ushindi chama chenu hatua ambayo ni utekelezaji wa wajibu wetu wa katiba kushinda dola zote mbili na kuongoza serikali zote mbili,”  alisema Dk. Shein.

Alisema umoja na mshikamano ndiyo msingi wa ushindi wa CCM hivyo aliwahimiza wanachama na wapenzi wa chama hicho kuendelea kuimarisha mshikamano wao na upendo miongoni mwao.

Dk. Shein ambaye pia ni Makamu Mwenyekiti wa Chama hicho, aliwaeleza viongozi hao kuwa ushindi wa chama hicho ni uthibitisho wa imani waliyonayo wananchi wa Zanzibar kwa Chama cha Mapinduzi na viongozi wake.

Akizungumza leo kwa nyakati tofauti na viongozi wa chama hicho wa ngazi ya mashina hadi wilaya katika Wilaya za Chake Chake na Mkoani, Dk. Shein alisema huu ni wakati muafaka kwa uongozi wa chama hicho katika ngazi zote kutekeleza majukumu yao inavyopaswa.

“Ni lazima viongozi na watendaji wa chama wafanye kazi kwa bidii   kufikia malengo na isiwe chama kinakuwa hai wakati wa ziara za viongozi tu,” Dk. Shein alisisitiza.

Alisema  chama hicho kina viongozi katika kila ngazi hivyo ni wajibu wa viongozi hao kuhakikisha   shughuli za chama zinafanyika ikiwamo ofisi zake kuwa wazi wakati wote kutoa huduma kwa wanachama na wananchi kwa jumla.

Alisisitiza kuwa kumalizika kwa uchaguzi uliopita ni kuanza kwa maandalizi ya uchaguzi ujao wa mwaka 2020 hivyo ni wakati muafaka kwa CCM kujizatiti na maandalizi hayo ili kupata ushindi wa kishindo.

Naye  Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Vuai Ali Vuai aliwapongeza wana CCM wa kisiwani Pemba kwa msimamo wao wa kukienzi na kuthamini chama chao bila ya kujali vituko wanavyofanyiwa na wapinzani kisiwani humo ili kuwakatisha tamaa.

Kauli ya Maalim Seif

Mei 14, mwaka huu akiwa Kisiwani Pemba, aliyekuwa mgombea urais wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupitia Chama cha Wananchi (CUF), Maalim Seif Sharif Hamad, alidai  Rais Dk. Shein hatamaliza miaka mitano kwani ataondolewa.

Hayo aliyasema alipozungumza na umati wana CUF waliojitokeza kumpokea nje ya nyumba yake iliyopo Jadida Wete, Kaskazini Pemba, wakati akitokea Unguja.

Alisema CUF inaungwa mkono na mataifa makubwa na zipo hatua mbalimbali ambazo wameelezwa kuwa wakizifuta watamwondoa rais aliyeko madarakani.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles