27.2 C
Dar es Salaam
Tuesday, April 23, 2024

Contact us: [email protected]

LWANDAMINA AANZA MOJA YANGA

Na THERESIA GASPER-DAR ES SALAAM

KOCHA Mkuu wa Yanga, George Lwandamina, ameamua kuanza moja kuzisuka safu zake tatu za kikosi chake, ili kuhakikisha zinatimiza malengo katika Ligi Kuu Tanzania Bara msimu huu.

Yanga ipo nafasi ya saba kwenye msimamo wa ligi hiyo ikiwa na pointi tano, baada ya kucheza mechi tatu, ikifanikiwa kushinda moja na kutoka sare mbili.

Ilianza kwa sare ya bao 1-1 na Lipuli FC, ikaibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Njombe Mji kabla ya kuilazimisha sare ya bao 1-1 na Majimaji.

Mwenendo huo unaonekana kutolivutia benchi la ufundi la timu hiyo lililo chini ya kocha George Lwandamina ambaye ameamua kukipika upya kikosi chake ili kiweze kufikia malengo yake ambayo ni kutetea ubingwa inaoushikilia.

Kikosi hicho kutoka Mitaa ya Twiga na Jangwani jijini Dar es Salaam, kesho kitashuka dimbani kukabiliana na Ndanda FC ukiwa ni mchezo wake wa nne wa Ligi Kuu msimu huu.

Katika mazoezi yaliyofanyika jana Uwanja wa Uhuru, Lwandamina,  aliamua kuwafungia kazi mabeki, viungo na washambuliaji wake  ili kuwafanya wawe bora zaidi.

Katika mazoezi hayo, kocha huyo alikigawa kikosi chake katika makundi manne na kuanza kutoa mafunzo.

Mabeki aliwanoa namna ya kuwazuia maadui, viungo walipewa jukumu la kupenyeza mipira kwa washambuliaji ambao walitakiwa kufunga mabao.

Kundi la washambuliaji liliundwa na Donald Ngoma, Ibrahim Ajib, Emmanuel Martin, Obrey Chirwa, Matheo Antony na Pius Buswita.

Lile la viungo lilikuwa na Papy Tshishimbi, Fiston Kayembe (yuko kwenye majaribio), Raphael Daud, Thaban Kamusoko, Pato Ngonyani na Maka Edward

Kundi la tatu lilikuwa la viungo wa pembeni ambao ni Juma Mahadhi, Geofrey Mwashiuya, Juma Makapu, Saidi Mussa, Baruan Akilimali na Maka Edward.

Katika kundi la nne likihusisha mabeki alikuwepo Andrew Vincent ‘Dante’, Mwinyi Haji, Kelvin Yondani, Abdallah Shaibu ‘Ninja’, Nadir Haroub ‘Cannavaro’.

Programu hiyo ilienda sambamba na kupigwa kwa mechi iliyohusisha vikosi viwili vya timu hiyo, cha kwanza kikiundwa na kipa Rostand Ngoma, Ajib, Chirwa, Raphael, Kamusoko, Abdul, Tshishimbi, Dante, Yondan na Gadiel.

Kikosi kingine kilikuwa na Mahadhi, Matheo, Kessy, Kayembe, Cannavaro, Haji, Buswita, Mwashiuya, Makapu, Maka na kipa wao, Ramadhani Kabwili.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles