33.2 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Lugola: Waliomteka Mo msako palepale

*Wengine waliopotea nao kuendelea kusakwa

Na RAMADHAN HASSAN, DODOMA

WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola amesema licha ya kupatika kwa mfayabishara Mohammed Dewji, serikali bado inaendelea kuwasaka watu walioshirikia katika tukio hilo.

Mo, alitekwa Oktoba 11, mwaka huu katika Hoteli ya Colessium iliyopo Masaki jijini Dar es salaam na kupatikana Oktoba 20 mwaka huu baada yatekelezwa na watekaji jirani na viwanja vya Gymkhana.

Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dodoma, Lugola, alisema bado msako unaendelea kuwatafuta watu waliomteka mfanyabiashara huyo.

“Niendelee kuwasihi ndugu zangu, mmekuwa mkitaka sana kujua tunaendeleaje kuwatafuta watekaji wa Mo, mimi nimeendelea kuwaambia kwamba Jeshi la Polisi linashughulika na matukio yote ambayo yametokea na kama kuna matukio yametokea ya mtu kupotea haonekani wote hao kwa ujumla wao tutayashughulikia.

“Wale ambao hatujawapata bado Jeshi la Polisi tunaendelea kuwatafuta hadi yule wa mwisho atakapotiwa mbaroni kwa hiyo ninyi msidhani kwamba hatuwatafuti kila mkiuliza mnaulizia Mo tu tunaomba muwe waangalifu.

“Mtaleta dhana kwamba watu wa kawaida wanapopata matatizo hawana thamani au pengine hatuwatafuti wale waliofanya uhalifu, mimi kama Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi siwezi kuacha hilo likaendelea,” alisema Lugola.

Waziri Lugola alisema Serikali ya Awamu ya Tano itawatafuta wale wote ambao waliotekwa bila kuangalia kama ni matajiri ama ni masikini.

“Serikali ya Rais Magufuli inamjali mnyonge kuanzia ngazi ya chini mpaka yule tajiri wa mwisho anapopata tatizo la usalama tunamjali kama tunavyomjali raia yoyote.

“Kwa hiyo kwa kifupi Jeshi la Polisi lipo imara bado tunaendelea kuwasaka wale wote ambao hatukuwapata katika matukio mbalimbali,” alisema

Waziri huyo wa Mambo ya Ndani ya Nchi, alitoa onyo kwa kwa watu ambao wamekuwa wakisema habari za watu kutekwa bila ya kuwa na ushahidi.

“Na ndiyo maana nitumie fursa hii, miongoni mwetu wapo Watanzania wa ajabu sana sijapata kuona, hawa baadhi tulipokuwa tunafanya msako, tulipokuwa tukitafuta watekaji wa Mo Dewji ndiyo hao hao waliokuwa wakisema jeshi letu halina uwezo, hatuwezi kufanikiwa.

“Lakini kwa sababu jeshi letu ni jeshi imara tulipohakikisha tumewanyima Oksijeni, pumzi watekaji tumeziba kila kona penalti imekabwa wenyewe walisalenda lakini hao hao Watanzania wanaanza kuuliza maswali,” alisema

Lugola alitoa tahadhari kwa kuwataka kukaa kimya na kuacha kuropoka kwani hatua kali zitachukuliwa juu yao.

“Nataka niwaambie kauli zao zisiendelee kutawala miongoni mwa Watanzania waliachie Jeshi la Polisi tunaendelea kuwasaka mpaka tuwatie mbaroni.

“Niendelee kusema hivi kweli ni kwa ajili hii midomo ya baadhi ya hawa watanzania hailipiwi kodi, haina VAT ndiyo maana kila kukicha ni kutoa kauli za upotoshaji, kauli za kejeli hivi kweli mnataka  ninyi baadhi yenu, maana tunawajua tuwatungie sheria ya VAT ya midomo yenu ili kila mnapozungumza tuweze kuwatoza kodi ili muweze kunyamaza.

“Lakini siku zenu si nyingi Serikali ya Magufuli sio ya kuchezewa na watu wachache, nawataka muache waacheni Watanzania waendelee kufurahia amani, nchi yetu ya tano kwa amani duniani,” alisema

ZIARA YA KUSHTUKIZA

Katika hatua nyingine Waziri Lugola, alifanya ziara ya kushtukiza katika kituo Kikuu  Kikuu cha Polisi Dodoma, na kukutana na madudu ikiwemo kukosekana kwa fomu za taarifa za mahabusu ambapo badala yake akakuta kataratasi za Bunge (Order Paper) zikitumika kuandikia taarifa hizo.

Pamoja na hali hiyo pia alibaini baadhi ya mahabusu wakiwa wamebambikiziwa kesi.

Waziri Lugola alifika majira ya saa tano asubuhi na moja kwa moja akapitiliza mapokezi na kupokelewa na askari aliyekuwepo aliyejitambulisha kwa jina la Godfrey Kasimba.

Mara baada ya askari huyo kujitambulisha,Waziri Lugola alitaka apewe fomu za kujazia taarifa za mahabusu ambapo askari huyo alimjibu kwamba hazipo na kumuonesha karatasi ambazo hutumiwa na bunge(Order paper) ambazo huzitumia kuandikia taarifa hizo.

“Naomba fomu  za kujazia taarifa za mahabusu,” alisema Waziri Lugola.

Hata baada ya kuomba karatasi hizo alijibiwa na askari Kasimba kuwa karatasi hizo hazipo.

“Mbona simuoni Mkuu wa kituo, nikukupa kituo wewe utaweza kufanya kazi,” alihoji Lugola.

Akimjibu, Kasimba alisema yupo tayari kufanya kazi hiyo lakini mkuu wa kituo amechelewa kutokana na kwenda kanisani.

Mara baada ya muda aliingia Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, Gilles Muroto akiwa na Mkuu wa Usalama Barabarani Mkoa wa Dodoma, Nuru Selemani na kuanza kujibu maswali ya waziri huyo.

Waziri Lugola aliingia mahabusu na kuanza kukagua makosa ya mtu mmoja mmoja kwa zaidi ya saa tatu.

Akizungumza na waandishi wa habari baada ya kumaliza ziara hiyo ya kushtukiza, Waziri huyo alisema amebaini baadhi ya mahabusu wamebambikiziwa kesi na wapo katika kituo hicho kwa muda mrefu.

Hivyo, aliwaagiza wakuu wa polisi nchini kuhakikisha wanafanya kazi zao kwa ueledi na kumaliza kasoro mbalimbali katika vituo vyao.

Pia aliwaagiza kutozuia raia kumtolea dhamana mtuhumiwa yeyote kwa kuwawekea masharti magumu ambayo yanasababisha ashindwe.

Licha ya hali hiyo alitoa onyo kwa maofisa wa polisi pamoja na wakuu wa polisi wa mikoa ambao wanashindwa kutekeleza maagizo ya waziri kwa madai kuwa ni maagizo ya kisiasa huku akisema kuwa wale ambao hawataki kutekeleza watashughulikiwa.

“Mimi ndiye Waziri wenu na maagizo ninayotoa siyo ya kisiasa, sasa RPC na maofisa ambao watapenda kuingia katika mkumbo wa kutokutekeleza maagizo ambayo nayatoa wakidhani ni maagizo ya kisiasa nitapambana nao.

“Na nimeisha mwandikia Inspekta Genelal wa Jeshi la Polisi Simon  Sirro kwa kumwelekeza kuwa wale ambao watashindwa kutekeleza maagizo yake wajulikane kuwa hawatoshi na hawawezi kula chungu kimoja na yeye na ikibidi wapishe mapema,” alisema Lugola.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles