27.5 C
Dar es Salaam
Friday, March 29, 2024

Contact us: [email protected]

Lugola: Sitasamehe polisi atakayeshiriki dawa za kulevya

FELIX MWAGARA  -ARUMERU

WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola, amepiga marufuku na kutoa onyo kali kwa magari ya polisi nchini kutumika kubeba au kusindikiza dawa za kulenya.

Lugola alisema wapo baadhi ya polisi wanatuhumiwa kufanya matukio ya kubeba bangi, mirungi pamoja na dawa aina mbalimbali za kulenya hapa nchini wakitumia magari ya Jeshi la Polisi  jambo ambalo ni kinyume cha sheria.

Akizungumza na wananchi katika mkutano wa hadhara uliofanyika Soko la Ngaramtoni wilayani Arumeru, mkoani Arusha jana mara baada ya kukabidhiwa gari la polisi lililokarabatiwa na Kampuni ya Friedkin Conservation Fund (CFC) ya hapa nchini kwa gharama ya shilingi milioni 15, alisema kitendo hicho kinalifedhehesha Jeshi la Polisi ambalo linatakiwa kuwa mfano wa kukabiliana na uhalifu.Kutokana na hilo alisema polisi yeyote akikamatwa kushiriki kufanya tukio hilo hatamwonea huruma kamwe, ataondolewa katika nafasi hiyo na kushtakiwa.

“Polisi wakikamatwa wanasindikiza au kubeba dawa za kulevya, polisi hao tutawafukuza kazi pamoja na kuwashtaki, gari hili la polisi ambalo limekarabatiwa na taasisi hii, litumike vizuri kwa kupambana na wahalifu na si vinginevyo,” alisema Lugola.

Aidha, Mbunge wa Viti Maalumu wa CCM wilayani humo, Amina Mollel, alimlalamikia Waziri Lugola akisema ndani ya wilaya hiyo kuna kesi ambazo zinachukua muda mrefu katika vituo vya polisi kwa kisingizio cha upelelezi kuwa haujakamilika hasa kesi za ubakaji ambapo alitoa namba ya faili mkutanoni hapo.

Katika hilo Lugola alimwagiza Mkuu wa Polisi wilayani humo (OCD) kutafuta faili la kesi zilizotajwa na mbunge huyo ili aweze kumletea katika mkutano huo.

Baada ya kutoa agizo hilo, OCD alileta faili hilo katika mkutano huo na kumkabidhi Mkuu wa Wilaya hiyo, ambaye pia ndiye Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama, Jerry Murro, ili aweze kumkabidhi Waziri Lugola na kutoa maelekezo zaidi.

Waziri Lugola yupo mkoani Arusha kwa ziara ya kikazi ambapo anatembelea wilaya zote za mkoa huo akifuatilia utendaji kazi wa taasisi zilizo chini ya wizara yake

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles