31.2 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Lowassa: Huu ni wakati wetu wa kukimbia

NA MWANDISHI WETU, TABORA

WAZIRI Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, amesema ni muhimu kwa Tanzania kukimbia kwa kasi ili kukabiliana na changamoto za maendeleo ya kisanyansi duniani.

Lowassa ambaye pia ni Mbunge wa Monduli (CCM), aliyasema hayo jana alipokuwa akihutubia katika sherehe za Jubilee ya miaka 25 ya uaskofu na miaka 40 ya upadri ya Askofu Paul Ruzoka wa Jimbo Kuu Katoliki la Tabora.

Kwa mujibu wa Lowassa, elimu ya Tanzania inakabiliwa na changamoto nyingi na kwamba njia sahihi ya kukabiliana na changamoto hizo ni kwenda na kasi ya maendeleo duniani.

“Ni wazi kwamba, mabadiliko haya makubwa yametufikisha mahali ambako sisi kama taifa tunapaswa kuchukua hatua za kuruka ili kuweza kukabiliana na kasi kubwa ya maendeleo yanayotokea duniani hivi sasa.

“Maendeleo hayo makubwa yanapaswa yawe darasa la kuirejesha Tanzania katika falsafa ya elimu ya kujitegemea kwani elimu hiyo inajenga misingi imara kwa wahitimu wanaomaliza shule na vyuo kuanzia kidato cha nne na kuendelea ili waweze kujiajiri au kuajiriwa katika sekta mbalimbali,” alisisitiza Lowassa.

Pamoja na hayo, Lowassa ambaye amekuwa mdau wa elimu nchini, alilipongeza Kanisa Katoliki kwa mchango mkubwa linaoutoa katika maendeleo ya elimu nchini.

Alisema kwamba, kanisa hilo limekuwa mstari wa mbele katika kusaidia kujenga misingi imara ya kupambana na maadui wakubwa wa maisha ya binadamu wakiwamo ujinga, umasikini na maradhi.

Pia, aliliomba kanisa hilo lishirikiane na Serikali na wananchi katika ulinzi na usalama kwa kuwa kuna dalili za kuvurugika kwa amani baada ya uwepo wa matukio ya ugaidi nchini.

Pia, Lowassa alimuomba Askofu Ruzoka aendelee kusaidia kutatua matatizo katika nchi za maziwa makuu zikiwamo Burundi ambako pameanza kuchafuka.

Awali, Rais wa Baraza la Maaskofu Tanzania (TEC), Mhashamu Askofu Tarcius Ngalalekumtwa, alimpongeza Askofu Ruzoka kwa kazi kubwa aliyoifanya katika kipindi cha miaka 25 ya uaskofu.

“Baba Askofu nakupongeza sana kwa mengi uliyoyafanya hususani kule Burundi ambako umesaidia kuleta amani na leo hii tunaye baba askofu kutoka Burundi,” alisema Askofu Ngalalekumtwa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles