24.7 C
Dar es Salaam
Tuesday, March 19, 2024

Contact us: [email protected]

LISSU ASHAURIWA KUTUNGA KITABU CHA MAISHA YAKE

ELIYA MBONEA Na ABRAHAMU GWANDU – ARUSHA

MBUNGE wa Singida Kaskazini, Tundu Lissu (Chadema), anatarajia kutunga kitabu kuhusu maisha yake.

Taarifa hiyo ilitolewa mjini hapa jana na kaka yake, Alute Mughwai, alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari.

Katika mkutano huo, Mughwai ambaye pia kitaaluma ni mwanasheria na msemaji wa familia, aliitisha mkutano huo ili pamoja na mambo mengine, kuelezea afya ya mbunge huyo anayetibiwa jijini Nairobi, Kenya.

“Kwa sasa anaendelea vizuri kutokana na matibabu anayoendelea kuyapata jijini Nairobi.

“Kuhusu mchakato wa kumpeleka kwenye matibabu zaidi nje ya Nairobi, tunaendelea na maandalizi ya safari hiyo ingawa siwezi kusema tutampeleka nchi gani.

“Lakini, habari njema iliyopo ni kwamba hatasafirishwa kwa ‘air ambulance’ na badala yake atasafiri kwa ndege ya abiria ya kawaida.

“Akiwa huko ughaibuni, tumemshauri atumie muda huo kuandika kitabu cha historia yake ili aeleze habari ya miaka ya 1990 ambapo mzee mmoja kutoka Moshi, alisafiri hadi Singida kumpaka mafuta,” alisema Mughwai.

Wakati huo huo, Mughwai alisema mdogo wake atakapopona, ataendelea kufanya siasa na kazi za uanasheria kwa nguvu zake zote.

“Bila kupepesa macho, ameniambia kwa kinywa chake, kwamba atakaporejea nyumbani, ataendelea kufanya kazi ya siasa na uanasheria kwa nguvu na ari kubwa.

“Hiyo ni pamoja na kuhakikisha waliotaka kutoa roho yake na washirika wao, wanashughulikiwa kikamilifu, ikiwa ni pamoja na kusimamia upelelezi wa tukio hilo kwa nguvu zake zote hadi wahusika wafikishwe mahakamani.

“Kuhusu matibabu yake, ni kama nilivyosema, kwamba yanaendelea vizuri na Alhamisi ya wiki iliyopita, alifanyiwa upasuaji mdogo uliokwenda vizuri na matumaini yetu na madaktari, ni kwamba huo ndiyo ulikuwa upasuaji wa mwisho kabla hajaanza hatua ya uangalizi na kufanyiwa mazoezi ya viungo.

“Lakini, pia tishio hilo la mauaji limemuweka kwenye ari kubwa na limemuimarisha kiroho na kimwili, ila tatizo linalomkabili kwa sasa ni upweke kwa sababu anakosa watu wa kuzungumza nao, wakiwamo wanahabari na kujua taarifa za matukio ya nyumbani.

“Kwa kuwa tunalitambua hilo, tunapokwenda Nairobi kumuona, tunampelekea magazeti mpaka ya udaku na huyasoma yote,” alisema Wakili Mughwai.

Akizungumzia baadhi ya mambo atakayoyafanya baada ya kurejea rasmi nchini, Mughwai alisema kuwa mdogo wake huyo atakwenda Hospitali ya Mkoa wa Dodoma kuwashukuru madaktari na wauguzi waliompatia huduma ya kwanza.

“Baada ya hapo, atakwenda nyumba za ibada kumshukuru Mungu kwa kumwepusha na kifo, lakini kwa kuwa sisi familia ni Waafrika, tutaangalia uwezekano wa kufanya tambiko kwenye makaburi ya wahenga wetu 76 waliofariki wakati wa vita ya kienyeji iliyopiganwa miaka 250 iliyopita.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
584,000SubscribersSubscribe

Latest Articles